Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ali amewapa pole Wanasimba wote baada ya jitihada za kuwania ubingwa ligi kuu msimu huu kufika tamati jana
Ahmed amesema licha ya machungu wanayopitia, hawapaswi kukata tamaa kwani mechi nne zilizobaki ni muhimu sana katika kuhakikisha wanamaliza katika nafasi ya pili
Ahmed amesema Simba lazima ijihakikishie tiketi ya kucheza ligi ya mabingwa msimu ujao kwani kama wataikosa nafasi hiyo maumivu yatakuwa makali zaidi
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Ahmed ameandika ujumbe huu;
"Leo ni usiku mgumu kwetu uliojaa maumivu na uchungu mkali
Lakini hatuna budi kukubali kuwa huu ndio ushindani
Kitu muhimu wana Simba ni kutambua kuwa kwetu ligi haijaisha
Tungali bado mioyo yetu inavuja damu kwa uchungu wa kukosa taji lakini hatuna budi kusimama imara tuipiganie Simba yetu imalize nafasi ya pili
Hii ndio nafasi pekee yenye thamani tuliyobakiwa nayo kwa sasa, inawezekana usione uzito wa nafasi hiyo lakini tukiiikosa ndio utagundua tumepoteza kitu kikubwa kiasi gani
Lets go wana Simba kila vita ina hatua zake tumepoteza hatua ya kwanza sasa tupambane tushinde ya hatua pili
Tukifanikiwa kushinda vita ya hatua ya pili, turudi kambini tujipange kuanza upya kwa msimu ujao"



