Kocha Mkuu wa Yanga, Miguel Gamondi amesema licha ya kuwa na msimu mzuri bado wana kazi ngumu mbele yao katika fainali ya kombe la Shirikisho la CRBD Bank dhidi ya Azam Fc
Katika fainali hiyo Yanga atakuwa ugenini mbele ya wenyeji Azam Fc, mchezo utakaochezwa Juni 2, mwaka huu uwanja wa New Amaan Complex, Visiwani Zanzibar, saa 2:15, usiku
Gamondi amesema anafurahi kufikia malengo yao kwa kutwaa taji la ligi pamoja na mchezaji wake Stephane Aziz Ki kufanikiwa kumaliza msimu akiwa kinara wa ufungaji bora
"Mwanzoni mwa msimu niliwaambia kuhusu Aziz Ki, kuwa ni mchezaji mkubwa na atafanya mambo makubwa anachukuwa tuzo ya mfungaji bora ni jambo la kujivunia. Licha ya yote lakini bado hatujamaliza kazi kubwa iliyopo mbele yetu ni fainali," amesema Gamondi
Amesema wana fainali ya Shirikisho dhidi ya Azam Fc, hautakuwa mchezo rahisi lakini anaimani na vijana wake watafanya vizuri na kufanikiwa kutwaa taji hilo ambalo wanalishikilia kwa misimu miwili mfululizo
"Msimu huu tumecheza vizuri, nimekuwa na timu bora, safu ya ulinzi, viungo na washambuliaji na tumefanikiwa kutoa mfungaji bora sasa tunataka kushinda taji la FA"
"Fainali ni kati ya timu mbili na mmoja apate ushindi. Yanga kwangu ni timu bora kwa hapa nchini na tunaenda kucheza fainali kwenye uwanja mzuri ambao unachezeka vizuri"
Gamondi ameeleza kuwa haitakuwa fainali rahisi kulingana na mechi ya mwisho walipokutana na Azam Fc, walipoteza hali ambayo hataki kuona inajirudia katika fainali hiyo