Kampuni ya SportPesa ambao ni Wadhamini wakuu wa klabu ya Yanga, leo wamekabidhi fedha za bonasi kwa klabu hiyo baada ya kufikia mafanikio yanayokidhi makubaliano ya kimkataba
Yanga imetwaa taji la Ligi Kuu, kombe la Shirikisho la CRDB pamoja na kufika robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari uliofanyika Masaki jijini Dar es saalam mapema leo, Mkurugenzi wa SportPesa Abbas Tarimba amewapongeza viongozi wa Yanga kwa kuongoza klabu hiyo kwa weledi ambao ni chachu ya mafanikio yao
SportPesa imeikabidhi Yanga hundi yenye thamani ya Tsh 537,500,000/- ambayo ni fedha za bonasi kutokana na mafanikio waliyopata msimu uliomalizika
"Yanga imekuwa ikiendeshwa kiuweledi. Hii inatokana na kuwa na Viongozi wenye njaa ya mafanikio. Nguvu hiyo imeifanya kuingia kwenye moja ya Klabu bora tatu barani Afrika"
"Nimpongeze sana Rais wa Yanga Injinia Hersi Said kwa jitihada zake kwa Klabu hii. Sisi kama Kampuni ya SportPesa vile vile tunampongeza Mdhamini na Mfadhili wa Yanga Ghalib Said Mohamed (GSM) kwa mchango wake mkubwa kwa Klabu hii. Bila shaka amefanya kazi kubwa, tunapenda salamu zetu zimfikie"
"Leo tunakabidhi mfano wa Hundi kwa Klabu ya Yanga kama BONUS ya mafanikio ya msimu. Hundi hii ina Thamani ya Tsh 537,500,000/= ambayo itawekwa kwenye akaunti za benki za Yanga"
"Nawashukuru pia Wachezaji na benchi wa Yanga kwa kile walichokifanya pale Zanzibar. Licha ya Wachezaji wetu wawili muhimu kukosa penati za mwanzo bado hawakupoteza malengo ya kuipambania nembo ya Klabu yetu" alisema Tarimba

