Wajumbe Simba upande wa Wanachama wamshukia Mo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 9th June 2024


Wajumbe Simba upande wa Wanachama wamshukia Mo

Baada ya taarifa za kujiuzulu kwa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi klabu ya Simba upande wa Mwekezaji, Wajumbe wa Bodi upande wa Wanachama wao wamegoma kujiuzulu

Jana viongozi wa Matawi ya Wanachama wa klabu ya Simba walikutana kwa dharura kujadili yanayoendelea ndani ya klabu ya Simba ambapo katika Mkutano huo walialikwa baadhi ya Wajumbe wa Bodi upande wa Wanachama

Akizungumza katika Mkutano huo, Mjumbe wa Bodi ya Simba CPA Issa Masoud alisema wamezisikia taarifa za Wajumbe wenzao upande wa Mwekezaji kujiuzulu ingawa amesema yeye binafsi hajathibitisha

CPA Masoud alikwenda mbali zaidi kwa kuelekeza kiini cha mgogoro huo ni baada ya Wajumbe hao kugoma kupitisha mapendekezo yaliyoletwa na Mwekezaji Bilionea Mohammed Dewji 'Mo' ambaye alitaka sehemu ya fedha ambazo amekuwa akizitoa kwa klabu ya Simba ziingie katika gharama za Uwekezaji (kwenye zile Bilioni 20)

"Fedha zote ambazo MO alikuwa anazitoa Simba Sc anazidai, na ameelekeza zibadilishwe ndio ziwe mtaji wake ambao anatakiwa autoe Simba Sports Club," alisema CPA Masoud

Fedha ambazo Mo amezitoa kwa klabu ya Simba tangu 2018 ni zaidi ya Bilioni 20 na hizi ni nje ya zile Bilioni 20 za uwekezaji ambazo ilielezwa ziliwekwa katika akaunti maalum

Aidha Mjumbe huyo ambaye ni mtaalam wa uchumi, aliongeza kuwa wakati Mo anatoa fedha hizo hakusema kama ni mkopo na hivyo hazikutolewa katika utaratibu wa Simba kukopeshwa

"Kama tunakopeshwa hizo hela kwani lazima tukope kwa MO Dewji?, Taasisi za fedha si zipo nyingi tunaweza tukakopa, Kwanza kama ni mkopo haujafuata taratibu alikopa nani na kwanini walikopa hizo hela, mkopo huo unawekwa kwa ajili ya aseti ipi, hapa ukiondoa udhamini maana ana udhamini,"alihoji CPA Masoud

CPA Masoud pia alisema wajumbe hao hawatambui Kamati zote zilizoundwa nje ya utaratibu pasipo kupitishwa na Bodi (rejea Kamati ya usajili iliyoundwa karibuni)

"Kamati yoyote ya Simba Sports Club inaundwa na Bodi, kwa hivyo basi kamati zote zilizoundwa nje ya bodi sisi hizo kamati hatuzitambui, na hata usajili utakaofanyika nje ya bodi sisi huo hatuutambui kwasababu tutakuwa tunakiuka utaratibu wa Simba SC."

"Sisi wenyewe tunasikia tu mtandaoni mara kamati ya usajili imeteuliwa, sasa sisi hizo kamati hatuzitambui kama bodi. Sisi tumepigania kwenye marekebisho ya katiba hii mpya tumpe nguvu M/Kiti wetu, na kwenye katiba hii M/Kiti wa Simba Sports Club atakuwa ndio Makamu M/Kiti wa Bodi, sisi tunataka utaratibu ufuatwe na mambo yafanyike kama kusajili wanachama wapya na mashabiki"


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.