Rais wa heshima klabu ya Simba, Bilionea Mohamed Dewji ametangaza kurejea kwenye nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba kufuatia ombi la Salim Abdallah 'Try Again' aliyejiuzulu nafasi hiyo jana Juni 11, 2024
Akizungumza kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Instagram, Dewji amesema lengo la kurejea ni kuweka mambo sawa baada ya klabu hiyo kuwa na mwenendo mbaya kwenye mashindano mbalimbali kwa kipindi cha miaka mitatu tangu aondeke kwenye nafasi hiyo
Aidha Dewji amesema amemuomba Try Again aendelee kuwa mjumbe wa Bodi, ombi ambalo limekubaliwa, na hivi karibuni atatangaza Wajunbe wengine watakaounda Bodi hiyo ili kuisimamisha upya Simba
"Ninarejea nikiwa na nguvu na ari mpya mpaka Simba itakaporejea kwenye hali yake ya kawaida"
"Nongozwa zaidi na ushabiki wa Simba, siyo uwekezaji, wala ufadhili wala udhamini. Sitaiacha Simba leo wala kesho," alisema Mo
Dewji ametaja mambo sita ambayo anaamini yamepelekea Simba kupoteza nguvu yake huku akiahidi kuyafanyia kazi
- Umoja: Hakuna umoja ndani klabu na kumekuwa na mgawanyiko uliotokana na makundi ya uchaguzi.
- Timu yenye ushindani: Benchi la ufundi halikuwa zuri hivyo kushindwa kutengeneza timu yenye ushindani.
- Usajili: Wachezaji wengi waliosajiliwa, viwango vyao havikuwa bora.
- Ukuaji wa wanachama: Eneo la mashabiki na wapenzi limedumaa hasa kutokana na kukwama kwa mchakato wa mabadiliko (transformation).
- Kutokuwepo kwa mkakati wa ukuzaji na uendelezaji wa vijana
- Miundombinu iliyoko Bunju kutokidhi mahitaji. Mohamed ameahidi kutatua changamoto hizo kwa kushirikiana na wenzake huku akiwataka wanasimba wote kuwa kitu kimoja, kumpa ushirikiano, kuzika tofauti zao na kuepuka migogoro.



