Klabu ya Azam FC imesema licha ya Pyramids ya Misri kuonekana kama kikwazo kwenye njia yao ya mafanikio ya michuano ya kimataifa, lakini malengo yao bado yapo pale pale ya kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika
Mwenyekiti wa klabu hiyo, Nassor Idrissa 'Father', amesema jana kuwa msimu huu wamejipanga kufanya vema na kwamba haijalishi ni mpinzani gani aliyekuwa mbele yao
Azam imepangwa kucheza dhidi ya APR ya Rwanda katika mechi ya raundi ya awali, Ligi ya Mabingwa Afrika, ikianzia nyumbani Agosti 16 hadi 18, kabla ya marudiano, Agosti 23 hadi 25, mwaka huu, na baada ya hapo itacheza na mshindi kati ya JKU ya Zanzibar dhidi ya Pyramids katika michezo ya raundi ya kwanza inayotarajiwa kuchezwa Septemba 13 na marudiano yake yatakuwa Septemba 20, mwaka huu
"Kihistoria hii ni mara yetu ya pili kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika, tuliwahi kucheza huko nyuma na tuliondolewa na El Merrikh ya Sudan, hii tunarudi kwa mara ya pili sasa, lengo letu ni kucheza hatua ya makundi, tukifika hatua hiyo sisi kama klabu tutakuwa hatuna deni kabisa, ila siyo kwamba tukifika tutasema imetoka tunajitoa, hapana, tutapambana ili kwenda mbele zaidi na tutakuwa tumekwenda juu ya malengo yetu"
"Tunaomba tu vijana wetu wasipate matatizo ya kiafya ili tutimize malengo yetu na tuna matumaini makubwa sana ya kufanya vema msimu huu na haijalishi wapinzani waliokuwa mbele yetu," alisema Father
Alisema pamoja na kwamba watu wanaizungumzia zaidi mechi yao dhidi ya Pyramids ambayo haijafika, lakini wao wanaiangalia APR kama ndiyo kikwazo chao, kwani wanatakiwa kwanza waitoe mashindanoni ndiyo waanze kuipigia mahesabu mechi inayofuata
"Ni kweli hatuna rekodi nzuri kwenye michuano ya kimataifa, ni kweli watu wanaiangalia zaidi Pyramids, lakini mbele yetu kwanza yupo APR, lazima kwanza tuwatoe ndiyo tufike huko, hatutaki kumfikiria mpinzani anayefuata kabla ya kucheza naye, haya mambo yalishatugharimu sana huko nyuma, kwa hiyo kwanza tumtoa yeye ndiyo twende huko kwa Pyramids, naye naamini tutamuondoa," alisema
Azam Fc imeweka kambi nchini Morocco kwa ajili ya kujiandaa na mikiki mikiki ya ligi na michuano ya ligi ya mabingwa inayoanza mwezi August 2024



