Red Arrows mabingwa Kagame Cup

Joel JJ By Joel JJ β€’ 21st July 2024


Red Arrows mabingwa Kagame Cup

Michuano ya Kombe la Kagame 2024 imefikia tamati kwa timu ya Red Arrows ya Zambia kutwaa ubingwa wa michuano hiyo baada ya kuifunga APR ya Rwanda kwa penalti 10-9 kwenye mchezo wa fainali uliopigwa kwenye Uwanja wa KMC, jijini Dar es Salaam

Red Arrows inakuwa timu ya kwanza kutoka nje ya Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kubeba taji hilo tangu michuano hiyo ilipoasisiwa mwaka 1967, baada ya dakika 120 za pambano hilo la fainali kumalizika kwa sare ya bao 1-1

Katika dakika 90 za kawaida, timu hizo zilimaliza kwa kufunga mabao hayo, Red Arrows ikianza kutangulia kupitia kwa Ricky Banda aliyetumia mpira kambani dakika ya 63 kabla ya Mamadou Sy kuchomoa bao hilo dakika ya 89 na kufanya mchezo kwenda kwenye muda wa ziada ambao pia zilishindwa kufungana

Ndipo zikaja penalti ambapo tano za mwanzo kila moja ikikwamisha wavuni na kufuatiwa na piga nikupige hadi penalti ya 10 ambapo APR ilipaisha ile ya mwisho na Red Arrows ikatupia nyavuni na kuipa timu hiyo ya Zambia taji hilo na kitita cha Dola 30,000 (zaidi ya Sh 80 Milioni)

Hii inakuwa ni mara ya kwanza timu ya kwanza ya Zambia kufika fainali za Kagame, lakini pia ya kwanza kutoka nje ya Ukanda wa Cecafa kutwaa taji hilo, kwani mara tatu tofauti timu kutoka Ukanda wa Kusini mwa Afrika (Cosafa) zilishatinga fainali, lakini ziliishia patupu kwa kufungwa

Timu ya kwanza kucheza fainali ya michuano hiyo ilikuwa ni Rio Tinto ya Zimbabwe mwaka 1982 ilipopoteza mbele ya AFC Leopards ya Kenya, kisha zikafuata timu za Malawi, ADMARC Tigers mwaka 1983 ilipofungwa pia na Leopards kwa mabao 2-1 na Big Bullets ilichezwa mwaka 2021 na kulala 1-0 na kwa Express ya Uganda.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.