Mabosi wa Simba wamelazimika kufungua tena mazungumzo kumsajili kiungo mshambuliaji wa AS Vita Elie Mpanzu ambaye unaweza kusema katika dirisha hili la usajili ndiye mchezaji ambaye tetesi za usajili wake zimezungumzwa kwa muda mrefu zaidi
Baada ya sintofahamu ya Kibu Denis aliyetorokea Ulaya, ni wazi Simba inalazimika kusajili mchezaji wa kuziba nafasi yake
Ili kupata mchezaji wa daraja la juu, Simba inalazimika kuangalia tena nje ya nchi uamuzi ambao pia utawalazimu kuachana na mchezaji mmoja zaidi wa kigeni
Jana tetesi za Simba kurejea tena kwa Mpanzu zikaanza kuvuma ambapo taarifa zilibainisha kuwa Simba iliongeza dau ili kuishawishi AS Vita kumuachia winga huyo ambaye kwa sasa ndiye mchezaji bora wa Vita
Wadadisi wa masuala ya usajili wanasema kuna nafasi kubwa Simba itafanikiwa kumsajili winga huyo ambaye tayari alishafikia makubaliano binafsi juu ya maslahi yake pale atakapojiunga na Simba
Pengine Mpanzu alipaswa kuwa mchezaji wa kwanza kusajiliwa na Simba katika dirisha hili lakini ilitokea sintofahamu kuhusu mkataba wake
Mwenyewe alisema amemaliza mkataba na AS Vita lakini klabu hiyo ikakanusha na kuthibitisha kuwa Mpanzu bado ana mkataba wa mwaka mmoja
Changamoto ikawa dau ambalo Vita wanataka ambapo Mnyama atalazimika kutoa zaidi ya Milioni 600 kununua mkataba wake wa mwaka mmoja uliobaki
Wakati huu Simba imerejea ikiwa 'serious' na pengine ile kiu ya Wanamsimbazi kumuona Mpanzu akivaa uzi wa Mnyama inaweza kufanikiwa



