Stars matumaini kibao DR Congo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 9th October 2024


Stars matumaini kibao DR Congo

Kaimu Kocha Mkuu, Suleiman Hemed Morocco, amesema watapambana dhidi ya DR Congo ili kupata ushindi kwani wanahitaji kufuzu kwa michuano ya Afcon 2025 itakayofanyika Morocco

Akizungumza jana kabla ya kupaa na ndege maalum ya serikali, iliyotolewa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, Morocco alisema wanafahamu kuwa wanakwenda kucheza mechi ngumu, lakini wamejiandaa kuhakikisha wanapata matokeo mazuri katika mchezo huo

Stars itajitupa kwenye Uwanja wa Stade des Martys jijini Kinshasa, kucheza na Timu ya Taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo Alhamisi saa 1:00 usiku kwa saa za Tanzania

Morocco alisema kwa sasa Stars inaweza kucheza na timu yoyote barani Afrika na kufanya vizuri kutokana na kuwa na wachezaji vijana, wenye uwezo mkubwa wakichanganyika na wazoefu

"Tunakwenda kucheza na timu nzuri, na wana mwendelezo kwenye ushindi wao, siyo rahisi haitokuwa mechi ya kitoto, lakini naamini na sisi tutakwenda kuleta upinzani ili tushinde mechi hiyo, kama tulishinda dhidi ya Guinea kwao kwa nini tusiifunge DR Congo? "

"Kwa sasa timu ya taifa inaweza kucheza na timu yoyote kwa sababu tuna wachezaji wazuri, vijana na wazoefu, tunakwenda kupambana kuhakikisha lengo letu mama la kufuzu AFCON linafanikiwa," alisema kocha huyo

Naye beki wa kushoto wa timu hiyo, Mohamed Hussein 'Tshabalala' alikiri kuwa wanakwenda kucheza na timu ngumu, yenye wachezaji wengi wanaokipiga nje ya Bara la Afrika, lakini na wao hawatokuwa wanyonge kwani wana maelekezo ya kufanya waliyopewa na walimu wao

"Tumejitahidi kupokea maelekezo ya walimu wetu kuelekea kwenye michezo yetu miwili dhidi ya DR Congo, sisi kama wachezaji tunakwenda kufuata kile tulichoelekezwa kwenye mechi hiyo, tunajua kuwa wenzetu wana wachezaji wazuri sana, wanacheza klabu kubwa nje ya Afrika, hivyo tunajua kama tunakwenda kucheza mchezo mgumu, lakini na sisi tumejiandaa kushinda ugenini," alisema


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.