Mshambuliaji wa Yanga Jean Baleke 'amejipakulia minyama' kwa kusema yeye ni mshambuliaji bora na hataacha urafiki wake na nyavu
Baleke aliyetua Yanga msimu huu kwa mkopo akitokea klabu ya TP Mazembe, ameanza maisha yake na Yanga kwa kusuasua
Baleke amesema kama mchezaji ataendelea kujifua ili awe bora zaidi na ataisaidia Yanga kila atakapopewa nafasi ya kucheza
"Mimi ni mfungaji bora, nitaendelea kupambana na kuisaidia timu yangu kila nitakapopata nafasi ya kucheza," alisema Baleke
Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi alimpa Baleke program maalum ya mazoezi kabla ya kuanza kumtumia baada ya kutoridhishwa na 'fitness' yake
Katika moja ya mahojiano yake, Gamondi alibainisha Baleke ni mshambuliaji mzuri lakini alihitaji kumuimarisha katika baadhi ya maeneo
Gamondi alisema ulikuwa ni mpango maalum ulioandaliwa kwa ajili ya mchezaji huyo ambaye wakati anajiunga na Yanga alikuwa na changamoto ya uzito na alitakiwa apungue kidogo ili aweze kuendana na kasi ya Yanga
"Tulimpa programu maalum ili kumuongezea wepesi wa kufanya uamuzi akiwa karibu ya lango na kufunga zaidi ya alivyozoeleka"
"Pia mjue kabisa Baleke ni mahiri zaidi kwa kufunga mabao ya kichwa kuliko miguu, tunataka awe na uwiano mzuri wa kufunga mabao ya aina zote”
"Mshambuliaji mzuri ni yule ambaye anaweza kufunga kwa mipira ya aina zote juu na chini, kwani kazi yake kubwa ni kuipa timu matokeo ndio maana tunamnoa zaidi, lakini sio kama nina tatizo naye, wachezaji wote kwangu ni wachapakazi, kikubwa natafuta matokeo zaidi kuliko jina la mtu," alisema Gamondi
Baleke tayari amekamilisha program maalum aliyokuwa amepatiwa na Gamondi alimtumia kwa takribani dakika 60 katika mchezo uliopita wa ligi kuu dhidi ya Pamba Jiji Yanga ikiibuka na ushindi wa mabao 4-0
Baleke ndiye aliyesababisha bao la pili lililofungwa Stephane Aziz Ki kupitia mkwaju wa penati baada ya kuvutwa ndani ya eneo la hatari
Angeweza kuondoka na bao lake siku hiyo kama sio uimara wa mlinda lango wa Pamba Jiji Yona Amos aliyeokoa moja ya michomo hatari iliyopigwa na Baleke mwanzoni mwa kipindi cha pili
Mwenyewe ameahidi kama atapata nafasi ya kucheza katika mchezo dhidi ya Simba Oktoba 19, basi atapeleka kilio kwa waajiri wake hao wa zamani