Mwenyekiti wa zamani wa klabu ya Simba Ismail Aden Rage amesema mlinda lango Moussa Camara alifanya makosa ya kibinadamu katika mchezo wa ligi kuu ya NBC dhidi ya Yanga uliopigwa Jumamosi iliyopita na Simba kufungwa bao 1-0
Rage amewaasa viongozi wa Simba wanaomtuhumu mlinda lango huyo kuwa amewahujumu, wamuombe radhi kwani tangu aliposajiliwa na timu hiyo amefanya kazi nzuri
"Mimi namuomba radhi Camara kwa tuhuma anazotupia kwani naamini hazina ukweli. Viongozi wangu wa Simba wanaomtuhumu wanapaswa kumuomba radhi pia kwani hawamtendei haki"
"Camara alifanya makosa kama binadamu, tunafahamu mpira ni mchezo wa makosa, Yanga wakatumia makosa hayo kutufunga"
"Haileti taswira nzuri pale kiongozi aliyehusika kusajili wachezaji anatoka hadharani kumtuhumu mchezaji kuwa amewahu"
"Wanasimba tunapaswa kukubali tumepoteza mchezo dhidi ya Yanga, wenzetu walikuwa na bahati, tusitafute mchawi kwenye hili"
"Kama sisi hatutaki kufungwa basi tuanzishe mashindano ya peke yetu ambayo yatashirikisha timu za Simba tu. Lakini kama sivyo basi tukubali tunapofungwa na tujipange ili tufanye vizuri mechi zinazofuata," alisema Rage
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba Cresentius Magori alimtuhumu Camara kuwa aina ya kosa alilofanya kupelekea Yanga kufunga bao halikubaliki
Magori alitishia kuzungumza na wanahabari kueleza alichoita sintofahamu nyuma ya kipigo cha Simba lakini baadae aliahirisha Mkutano huo baada ya kupokea ushauri



