Mshambulizi Robert Lewandowski alifunga bao katika kila kipindi na kusaidia Barcelona kupata ushindi mnono wa 5-2 dhidi ya Red Star Belgrade kwenye Ligi ya Mabingwa Jumatano
Huo ulikuwa ushindi mwingine mnono kwa vinara wa LaLiga Barcelona ambao wako katika kiwango bora, wakifunga mabao 24 katika ushindi sita mfululizo katika michuano yote, ikiwa ni pamoja na kuwazaba Bayern Munich na Real Madrid
Barca walipanda hadi nafasi ya sita kwenye jedwali la timu 36 za Ligi ya Mabingwa wakiwa na pointi tisa. Red Star wamo katika nafasi ya 35 bila pointi katika michezo minne
Meneja Hansi Flick alifanya mabadiliko mawili kwa timu ya Barcelona ambao waliwashinda wapinzani wao Espanyol 3-1 kwenye LaLiga Jumapili, na kumpa kiungo Mholanzi Frenkie De Jong mwanzo wake wa kwanza tangu apone jeraha la kifundo cha mguu
Iliwachukua Wahispania hao dakika 13 pekee kufunga bao la kwanza wakati beki Inigo Martinez alipofunga kwa kichwa mpira wa faulo uliopigwa na Raphinha dakika ya 13
Red Star wakarejea mchezoni kupitia Silas ambaye alivunja mtego wa kuotea wa Barca na kuisawazishia Red Star kwa shuti kali
Barca waliendelea kutawala mchezo na kushikilia mpango wao wakiwashinikiza wenyeji na kutengeneza nafasi kadhaa kabla ya Lewandowski kuachia shuti kali la dakika ya 43 na kuongeza uongozi wa Barca
Kipindi cha pili, Lewandowski aliongeza lake la pili likiwa la tatu kwa Barca baada ya krosi nzuri ya Jules Kounde, na dakika mbili baadaye Raphinha akaongeza la nne
Fermin Lopez aliyetokea benchi akatoa pasi nyingine kwa Kounde kuongeza bao la tano
Milson akarudisha bao moja kwa Crvena Zvezda lakini haikutosha kuzuia kipigo hicho kikubwa katika uwanja wa nyumbani
Timu hiyo ya Serbia imesalia bila pointi baada ya kipigo hicho kikali, huku Barcelona wakiwa na pointi tisa na wako mbioni kutinga raundi inayofuata



