Barca yaendeleza ubabe Ulaya

Joel JJ By Joel JJ β€’ 7th November 2024


Barca yaendeleza ubabe Ulaya

Mshambulizi Robert Lewandowski alifunga bao katika kila kipindi na kusaidia Barcelona kupata ushindi mnono wa 5-2 dhidi ya Red Star Belgrade kwenye Ligi ya Mabingwa Jumatano

Huo ulikuwa ushindi mwingine mnono kwa vinara wa LaLiga Barcelona ambao wako katika kiwango bora, wakifunga mabao 24 katika ushindi sita mfululizo katika michuano yote, ikiwa ni pamoja na kuwazaba Bayern Munich na Real Madrid

Barca walipanda hadi nafasi ya sita kwenye jedwali la timu 36 za Ligi ya Mabingwa wakiwa na pointi tisa. Red Star wamo katika nafasi ya 35 bila pointi katika michezo minne

Meneja Hansi Flick alifanya mabadiliko mawili kwa timu ya Barcelona ambao waliwashinda wapinzani wao Espanyol 3-1 kwenye LaLiga Jumapili, na kumpa kiungo Mholanzi Frenkie De Jong mwanzo wake wa kwanza tangu apone jeraha la kifundo cha mguu

Iliwachukua Wahispania hao dakika 13 pekee kufunga bao la kwanza wakati beki Inigo Martinez alipofunga kwa kichwa mpira wa faulo uliopigwa na Raphinha dakika ya 13

Red Star wakarejea mchezoni kupitia Silas ambaye alivunja mtego wa kuotea wa Barca na kuisawazishia Red Star kwa shuti kali

Barca waliendelea kutawala mchezo na kushikilia mpango wao wakiwashinikiza wenyeji na kutengeneza nafasi kadhaa kabla ya Lewandowski kuachia shuti kali la dakika ya 43 na kuongeza uongozi wa Barca

Kipindi cha pili, Lewandowski aliongeza lake la pili likiwa la tatu kwa Barca baada ya krosi nzuri ya Jules Kounde, na dakika mbili baadaye Raphinha akaongeza la nne

Fermin Lopez aliyetokea benchi akatoa pasi nyingine kwa Kounde kuongeza bao la tano

Milson akarudisha bao moja kwa Crvena Zvezda lakini haikutosha kuzuia kipigo hicho kikubwa katika uwanja wa nyumbani

Timu hiyo ya Serbia imesalia bila pointi baada ya kipigo hicho kikali, huku Barcelona wakiwa na pointi tisa na wako mbioni kutinga raundi inayofuata


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.