Wakati ligi ikisimama kupisha kalenda ya FIFA, wawakilishi wa Tanzania katika mashindano ya klabu ya CAF hatua ya makundi Yanga na Simba, zimerejea mazoezini leo kwa ajili ya maandalizi ya mechi zitakazopigwa mwishoni mwa mwezi huu
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe amesema wawakilishi hao wa Tanzania katika michuano ya ligi ya mabingwa, wataanza na program ya mazoezi ya Gym majira ya saa 6 mchana
"Focus yetu kwa sasa tumeielekeza kwenye ligi ya mabingwa mchezo dhidi ya Al Hilal ambao utachezwa Novemba 26 katika uwanja wa Benjamin Mkapa"
"Timu inarejea mazoezini leo ambapo mchana tutakuwa na 'session' ya Gym pale Gymkhana"
"Tunakwenda kujiandaa kikamilifu kuelekea mchezo dhidi ya Al Hilal, mchezo huu tunautaka kwelikweli," alisema Kamwe
Nae Meneja Habari na Mawasiliano wa klabu hiyo, Ahmed Ally, amesema wachezaji watakaoanza mazoezi leo ni ambao hawatokwenda kwenye timu zao za taifa ambazo zinapambana kwa ajili ya kusaka tiketi ya kucheza fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, zitakazofanyika nchini Morocco
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Ahmed alisema baada ya mapumziko ya siku nne ambayo wachezaji wa timu hiyo waliyapata baada ya kucheza mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya KMC na kushinda mabao 4-0, kwenye Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam, Jumatano iliyopita, wachezaji wa timu hiyo wanarejea rasmi mazoezini, Uwanja wa Mo Arena, Bunju, Dar es Salaam kujiandaa na mchezo huo chini ya kocha raia wa Afrika Kusini, Fadlu Davids
"Kikosi kinarejea mazoezini leo Jumatatu baada ya siku nne za mapumziko, tukiliangalia Kombe la Shirikisho tuna uwezo wa kufanya vizuri msimu huu kwa mambo mawili"
"Kwanza kuanza michuano na ushindi mnono na pia tunaweza kuwa ndiyo klabu itakayokuwa inajaza mashabiki wengi zaidi kuliko zingine zinazocheza michuano hii katika michezo yote, na hili kwa mashabiki wa Simba linawezekana, deni litakalobaki ni kwa wachezaji wetu kupambana kutuletea ushindi tu," alisema Ahmed



