Kamati ya usimamizi na uendeshaji wa Ligi ya Bodi ya Ligi, imeitoza klabu ya Azam Fc faini ya Sh. 3,000,000 (milioni tatu) kwa kola la kuzuia wapigapicha wa mdhamini mwenye haki za matangazo ya runinga, Azam TV kurekodi picha jongeo wakati timu hiyo ikiingia katika uwanja wa Azam Complex, kuelekea mchezo dhidi ya Yanga
Kulingana na taarifa ya Kamati, kitendo hicho ni uvunjifu wa masharti ya udhamini wa Ligi Kuu ya NBC, jambo ambalo ni kinyume na kanuni
Adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 16:1(1.7) ya Ligi Kuu kuhusu Udhamini
Kamati hiyo pia imemfungia mechi tatu aliyekuwa kocha mkuu wa klabu ya Yanga, Miguel Gamondi na kutozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) kwa kosa la kumsukuma na kumuangusha chini kocha wa viungo wa klabu ya Singida Black Stars, Sliman Marloene, baada ya mabishano yaliyotokea wakati timu hizo zikienda mapumziko katika mchezo dhidi ya Singida BS kwenye uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 45:2(2.1) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Makocha
Kamati pia imefuta adhabu ya kadi ya manjano aliyoonyeshwa mchezaji Ibrahim Abdullah wa klabu ya Yanga katika mchezo dhidi ya Coastal Union, baada ya kujiridhisha kupitia picha jongeo na taarifa za wataalam kuwa mchezaji huyo hakustahili adhabu hiyo
Uamuzi huo ni kwa kuzingatia Kanuni ya 12:8 ya Ligi Kuu kuhusu Usimamizi wa Ligi
Klabu ya Singida Black Stars imetozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) kwa kosa la kuingilia mazoezi ya klabu ya Yanga siku moja kabla ya terehe ya mchezo baina ya timu hizo
Timu ya Singida iliingia kwenye uwanja wa New Amaan Complex katika muda wa kikanuni wa klabu ya Yanga kufanya mazoezi, jambo ambalo lilivuruga programu ya mazoezi hayo ya Yanga ambalo yalikuwa yakiendelea, kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:45 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo