Usiku wa leo vinara wa ligi kuu ya NBC, Simba wataondoka jijini Dar es salaam kuelekea Mwanza kwa ajili ya mchezo wa ligi kuu dhidi ya Pamba Jiji. Mchezo huo utapigwa Ijumaa, Novemba 22 katika uwanja wa CCM Kirumba
AKizungumza na wanahabari mapema leo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba Ahmed Ali alisema msafara wa Simba utakaoondoka utajumuisha wachezaji ambao walikuwa katika majukumu ya timu za Taifa
Ahmed alithibitisha wachezaji Shomari Kapombe, Mohammed Hussein, Aishi Manula, Kibu Denis na Moussa Camara watakuwa sehemu ya kikosi hicho kitakachosafiri huku mshambuliaji Steven Mukwala aliyekuwa na timu ya Taifa ya Uganda akitarajiwa kuungana na Simba jijini Mwanza mapema Alhamisi
Aidha kiungo Yusuph Kagoma na winga Joshua Mutale hawatakuwa sehemu ya kikosi cha Simba kinachosafiri wakiwa ni majeruhi
Simba inakwenda Mwanza ikiwa ndio vinara wa ligi kuu wakikusanya alama 25 baada ya mechi 10 alama moja mbele ya watani zao Yanga wanaoshika nafasi ya pili
Simba inatarajiwa kutumia mchezo dhidi ya Pamba kama sehemu ya maandalizi yake kuelekea mchezo wa kombe la Shirikisho hatua ya makundi dhidi ya Bravos utakaopigwa Jumatano, Novemba 27 katika uwanja wa Benjamin Mkapa



