Kocha Mkuu wa Simba Fadlu Davids amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa kwanza hatua ya makundi kombe la Shirikisho dhidi ya Bravos Fc ambao utapigwa kesho Jumatano katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Akizungumza katika mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Fadlu amesema wamekuwa wakijiandaa na mchezo huu tangu wakati wa mapumziko ya kalenda ya FIFA, leo watakamilisha maandalizi tayari kwa mchezo huo
"Niseme sisi tupo tayari kwa mchezo huu. Tulianza maandalizi ya mechi hii wakati wa mapumziko ya kalenda ya FIFA. Tuko hatua ya mwisho kwa ajili ya kuongeza na kurekebisha vitu vichache vya kiufundi"
"Tumejipanga na tutahakikisha tunapata ushindi katika mechi yetu ya kwanza nyumbani," alisema Fadlu
Aidha Fadlu amebainisha kuwa anatambua mchezo hautakuwa mwepesi kwa sababu Bravos sio timu inayofungika kirahisi hivyo atahitaji kila mchezaji kujituma na kufuata mpango wa mchezo huku akiwataka mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanja wa Benjamin Mkapa hapo kesho
"Matatarajio yetu ni kupata alama tatu japo sio rahisi maana tunaujua ubora wa FC Bravos, tutatumia mbinu zetu ili kupata matokeo ya ushindi"
"Tunacheza na timu ngumu mechi yetu ya kwanza, tunahitaji nguvu ya mashabiki na nina imani Benjamin Mkapa itajaa," aliongeza Fadlu



