Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amewashukuru mashabiki waliosafiri kwa wingi kutoka jijini Dar es salaam na maeneo mengine kuelekea Ruangwa kuiunga mkono Yanga katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Namungo Fc utakaopigwa kesho Jumamosi katika uwanja wa Majaliwa
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari kuelekea mchezo huo, Ramovic amesema ni deni kubwa kwao kuhakikisha wanawapa furaha mashabiki wao kwa kushinda mchezo huo
Zaidi ya mabasi 10 yameondoka jijini Dar es salaam leo kuelekea Ruangwa kuipa sapoti Yanga katika mchezo huo
"Kwakweli ni jambo la Kujivunia sana, Nawashukuru sana mashabiki wa Yanga wanaotoka Dar es Salaam leo usiku na Wanayanga Wote wanaokuja Kuisapoti timu yetu hapo kesho, mimi na Wachezaji wangu tunapaswa kuwalipa Furaha, Wameonesha Moyo na Mapenzi ya Dhati, tunajiandaa kuirejesha furaha yao," alisema Ramovic
Akizungumzia maandalizi ya kikosi chake, Ramovic amesema wako tayari na wanachohitaji ni kushinda mchezo huo unaotarajiwa kuwa mgumu
"Tuna mchezo mgumu na muhimu sana hapo kesho, katika maandalizi yetu mpaka sasa kila kitu kipo vizuri, tunafahamu Namungo wana wachezaji wazoefu lakini sisi hatupo hapa kutafuta kingine zaidi ya alama tatu," alisema
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, Denis Nkane amesema wanakwenda kwenye mechi hiyo huku wakifahamu deni walilonalo baada ya kupoteza mechi zilizopita
"Sisi kama Wachezaji tunatambua umuhimu wa alama tatu kwenye Ligi, tumekaa chini na kuzungumza wapi kwa Kuboresha, tunamsikiliza Mwalimu na kujituma kwa dhati ili kuhakikisha tunapata matokeo mazuri, mchezo wa kesho ni mgumu lakini tupo kwaajili ya Kupambana na kushinda"
"Kwanza niwapongeze Wanayanga kwa mapenzi wanayoonesha, Nimesikia Leo wanasafiri kutoka maeneo mbalimbali na kuja kutusapoti, hili ni deni kwetu na tunapaswa Kulilipa, niwaombe Wanayanga wa Ruangwa nao waje kutusapoti kesho, tupo hapa kwa ajili ya kushinda," alisema



