Aliyekuwa mlinda lango wa Coastal Union Vumiley Matampi amesema sababu iliyopelekea avunje mkataba wake na klabu hiyo ni madai ya malimbikizo ya mishahara
Matampi ambaye ndiye kipa bora wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita akimpindua Djigui Diarra wa Yanga aliyebeba tuzo hiyo misimu miwili mfululizo, amesema sio rahisi kwake kufanya kazi huku akiwa halipwi stahiki zake
Mkongomani huyo aliyejiunga na Coastal Union Agosti 2023, mkataba wake ulitarajiwa kumalizika mwisho wa msimu huu baada ya msimu uliopita kutoa mchango wake mkubwa katika kuifanikisha timu hiyo kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika
Jana klabu ya Coastal Union ilitoa taarifa ya kuvunja mkataba wake na kumtakia kila la kheri katika safari yake ya soka
"Nilipewa barua wiki iliyopita na kwangu naona ni uamuzi mzuri tu ambao klabu imefikia kwani sikuwa napata haki yangu kama ilivyotakiwa. Sijalipwa mshahara wangu miezi mitatu, suala ambalo sio zuri kwa upande wangu, niko tayari sasa kwa changamoto mpya," alisema Matampi