Kocha Yanga matumaini kibao Congo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 13th December 2024


Kocha Yanga matumaini kibao Congo

Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amewashukuru mashabiki wa timu hiyo waliosafiri kwa basi kutoka Tanzania hadi Lubumbashi DR Congo kuishangilia timu yao kwenye mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe utakaopigwa kesho

Akizungumza na wanahabari kuelekea mchezo huo, Ramovic amesema ujio wa mashabiki hao umewaongezea hamasa wachezaji wake ambao anaamini kesho watapambana ili kuhakikisha wanawapa furaha

"Ni jambo kubwa sana ambalo Mashabiki wa Yanga wamelifanya, kusafiri kwa Basi kutoka Dar Es Salaam mpaka hapa Lubumbashi siyo rahisi"

"Ni faraja kwetu na inatupa motisha ya kuwa tuna watu wanaotupa moyo na kutufanya tusiyumbe, kwakweli nachoweza kusema ni kwamba tupo hapa kwaajili ya kuwapa furaha, timu nzima inatambua umuhimu wa mashabiki wetu, panapo majaaliwa kesho tutapambana kuhakikisha tunawafurahisha Wananchi," alisema Ramovic

Akizungumzia maandalizi ya kikosi chake, Ramovic amesema wamejiandaa kufanya vizuri katika mchezo huo ambao anatarajia utakuwa mgumu

"Malengo yetu ni kuonesha uwezo wetu na kufanya vizuri kesho, Haijalishi wapinzani wetu wakoje. Sisi tunafahamu TP Mazembe ni timu kubwa na ina Wachezaji wazuri hivyo kesho tutashuhudia mechi nzuri sana"

"Nafahamu kuwa mchezo wa mwisho hapa Congo Yanga ilishinda lakini hatuwezi kuzungumzia yaliyopita, tunautazama mchezo wa kesho kama mchezo mpya na tupo tayari kwa changamoto hii," alisema

Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, kiungo Maxi Nzengeli amesema wachezaji wako tayari kuonyesha ubora wao katika mchezo wa kesho na lengo ni kushinda

"Tunamshukuru Mungu tumefika salama, tupo hapa Lubumbashi kwaajili ya kupambana, ni kweli hatujashinda mechi zetu za mwanzo lakini haimaanishi tukae vichwa chini, huu ni muda wa kurudi juu na kuwapa furaha wananchi, tunatambua ukubwa wa Mazembe lakini tutapambana kwaajili ya kushinda kesho"

"Tunasema asante kwa mashabiki wa Yanga siyo rahisi kusafiri kwa basi mpaka hapa, haitakuwa rahisi lakini tunawahakikishia tutapambana sana kwaajili yao, Tunashukuru sana kwa kujitoa kwa ajili ya timu," alisema Maxi


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.