Simba imeendelea kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya leo kuichapa Singida BS bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa CCM LITI, Singida
Bao pekee la ushindi katika mchezo huo lilifungwa na Fabrice Ngoma katika dakika ya 42 akimalizia kwa kichwa mpira wa kona uliopigwa na Jean Charles Ahoua
Hilo lilikuwa bao la tatu kwa Ngoma msimu huu huku Ahoua akitoa assist yake ya tano
Simba iliuanza mchezo huo kwa kasi na pengine ingeweza kufunga bao mapema kama sio uimara wa mlinda lango Metacha Mnata na safu yake ya ulinzi
Kipindi cha pili kocha mkuu wa Simba Fadlu Davids alibadili mbinu za uchezaji wa kikosi chake ambapo akiongeza nguvu katika kujilinda na kutumia mashambulizi ya kujibu
Ahoua nusura aiongezee Simba bao la pili baada ya pasi ya Steven Mukwala lakini Metacha akaokoa mchomo mkali wa Ahoua ndani ya 18
Ni alama tatu muhimu kwa Simba ambazo zinawaweka kileleni mwa msimamo wa ligi wakifikisha alama 40 na hivyo kufunga mwaka 2024 Mnyama akipigwa na baridi kali pale juu



