Shirikisho la Soka barani Afrika CAF limetangaza kuisogeza mbele michuano ya mataifa bingwa ya Afrika CHAN hadi Agosti mwaka huu
Taarifa ya shirikisho hilo imebainisha kwamba wameahirisha michuano hiyo licha ya waandaaji ambao ni Kenya, Tanzania na Uganda kufanya vema katika maboresho ya viwanja, hoteli, hospitali na miundombinu na vifaa vingine kwa ajili ya kuandaa michuano hiyo
Hata hivyo wataalam wa Ufundi na Miundombinu wa CAF ambao baadhi yao wapo kwenye nchi hizo za Afrika Mashariki wamelishauri shirikisho hilo kuwa muda zaidi unahitajika kuhakikisha miundombinu na vifaa vipo kwenye viwango vinavyohitajika zaidi ili michuano hiyo ifanikiwe ipasavyo
Rais wa CAF, Dk Patrice Motsepe amewashukuru Marais William Ruto wa Kenya, Dk Samia Suluhu Hassan wa Tanzania na Yoweri Museveni wa Uganda kwa uongozi wao, kujitolea na maendeleo mazuri yaliyofikiwa hasa kwenye ujenzi wa miundombinu
Licha ya michuano hiyo kusogezwa mbele shughuli ya upangaji wa ratiba ya michuano hiyo itafanyika kesho kuanzia saa 2:00 usiku Mjini Nairob, Kenya lakini tarehe rasmi ya kuanza michuano hiyo itatajwa baadae



