Mshambuliaji mpya wa Singida Black Stars, Eliuter Mpepo amefichua kilichomkwamisha kutua Tabora United katika dirisha la usajili la Januari kuwa ni kuchelewa kuwekewa dau la usajili jambo lililomfanya kubadili uamuzi licha ya kupewa mkataba wa awali
Mpepo ambaye ni mmoja wa wachezaji wa Singida Black Stars inayonolewa na Hamdi Miloud, alisema kuchelewa kwa usajili kulimfanya kuangalia fursa nyingine baada ya kupewa ofa kutoka klabu tofauti
Mchezaji huyo ambaye aliwahi kuchezea Trident ya Zambia alikofunga mabao saba na kutoa asisti tano alieleza kuwa aliona ni bora ajiunge na Singida Black Stars
"Nilikuwa na mazungumzo na Tabora United na walikuwa wanataka kunisajili, lakini kutokana na kuchelewa kuweka dau langu nilikuwa na fursa nyingine nzuri," alisema
"Niliamua kuchukua hatua ya kuhamia Singida Black Stars kwa sababu niliona ni sehemu bora kuendelea kuonyesha uwezo. Hapa nipo na furaha na najiandaa kutoa mchango mkubwa kwenye timu hii," alisema Mpepo
Mpepo ameunga na mshambuliaji raia wa Ghana Jonathan Sowah ambaye pia amesajiliwa na Singida Black Stars katika dirisha dogo



