Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amesema wamejiandaa kwa mechi ngumu ya ligi kuu dhidi ya Kagera Sugar ambayo itapigwa leo Jumamosi katika uwanja wa KMC Complex
Akizungumza katika Mkutano na wanahabari jana, Ramovic alisema Kagera Sugar ni timu ngumu na watahitaji kuwa bora katika mchezo huo ili kuibuka na ushindi
Ramovic alisema dhamira ya Yanga ni kushinda kila mchezo ili kurudi kileleni mwa msimamo wa ligi, hivyo watapambana ili kushinda mchezo huo
"Tunafahamu utakuwa mchezo mgumu hivyo tunapaswa kucheza vizuri zaidi na kiukweli tunawaheshimu sana Kagera Sugar, Tunajua watakuja vizuri hasa kwa Kujilinda zaidi hivyo tunapaswa kutumia nafasi tutakazozitengeneza"
"Lengo letu kubwa ni kupata alama tatu kesho, sisi tunatazama zaidi mechi zetu na tuna jukumu la kushinda kila mchezo ili kurudi kileleni, tunajua ubora wa Kagera Sugar hivyo tuna jukumu la kucheza kwenye ubora wetu wa kila siku"
"Tuna mechi 15 mbele yetu, tunakwenda kucheza dhidi ya timu shindani kama tulivyo sisi, tunahitaji kushinda mechi zetu pasipo kuangalia matokeo ya wengine ili kuwa mabingwa," alisema Ramovic
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, beki Nickson Kibabage alisema wanatambua mechi dhidi ya Kagera Sugar itakuwa ngumu, wamejipanga kucheza kwa kumuheshimu mpinzani na muhimu kwao ni alama 3
"Kwa upande wetu sisi tumejiandaa vizuri na kila mchezaji anafahamu umuhimu wa Mchezo wa Kesho. Kikubwa ni kwamba tunawaheshimu sana Kagera Sugar kwasababu wana timu nzuri inayoleta Ushindani kwenye Ligi"
"Watakuja kuonesha ubora wao hivyo tunaamini utakuwa mchezo mzuri, Wananchi wategemee mazuri kutoka kwetu," alisema