Kocha Mkuu wa Simba Fadlu Davids amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Namungo Fc ambao utapigwa leo Jumatano, Februari 19 katika uwanja wa Majaliwa huko Ruangwa
Akizungumza jana katika Mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Fadlu amesema wanakwenda kukabiliana na timu ngumu ambayo ni imara katika safu ya ulinzi hivyo mpango wa mechi hiyo ni kutengeneza mashambulizi mengi na kutumia kila nafasi
Fadlu ameeleza kuridhishwa na kiwango cha kikosi chake katika mechi zilizopita akiwa na imani wataendeleza ubora wao katika mchezo huo
"Tumekuwa na muda wa kutosha kujiandaa na mchezo dhidi ya Namungo Fc, tuko tayari kwa mchezo huu"
"Nafurahi tumeendelea kuimarika na kuwa bora kutoka mechi moja hadi nyingine"
"Kesho (leo) tunakwenda kukabiliana na mpinzani mgumu mwenye safu nzuri ya ulinzi hivyo tutapaswa kuwa kwenye ubora wetu katika ushambuliaji"
"Malengo yetu ni kuona tunashinda mchezo huu ambao nafahamu hautakuwa mwepesi," alisema Fadlu
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake mlinzi wa kulia David Kameta 'Duchu' amesema morali ya wachezaji iko juu na malengo yao ni kuibuka na ushindi mnono
"Morali ya wachezaji wote iko juu kuelekea mchezo huo. Tunafahamu msimu uliopita hatukupata ushindi katika uwanja wa Majaliwa, tunalijua hilo hivyo tumejiandaa kufanya vizuri"
"Sasa tuna walimu tofauti na msimu uliopita, kitu kikubwa tunakwenda kupambana malengo yetu ni kupata alama tatu katika kila mchezo," alisema