Kampuni ya Kimataifa ya kutengenza vifaa vya Michezo Diadora ndiyo itakayotengeneza jezi za klabu ya Simba baada ya kuingia ushirikiano na kampuni ya Jayrutty
Akizungumza katika Makao Makuu ya Diadora ukanda wa SADC huko Afrika Kusini, Afisa Mtendaji Mkuu wa Jayrutty, Joseph Rwegasira amesema leo wametimiza moja ya ahadi waliyotoa kuipeleka Simba anga za Kimatifa
Diadora imefanya kazi ya kutengeneza vifaa vya micheza vya klabu kubwa barani Ulaya ikiwema klabu ya AS Roma
"Wakati tunatangazwa kuingia mkataba huu na kutengeneza vifaa vya Simba kuanzia msimu ujao niliahidi. Kutokana na ukubwa wa Simba ni wakati wa kwenda kimataifa na leo tupo makao makuu ya Diadora ukanda wa SADC na kwa mara ya kwanza tunakwenda kutangaza ushiriki wa pamoja kati ya Simba, Jayrutty na Diadora," alisema
Nae Mtendaji Mkuu wa Diadora Afrika Kusini Mr. Yusuf Vadi amesema ni furaha kwao kufanya kazi na klabu ya Simba wakiahidi kutengeneza jezi bora
"Tumefurahi kupata nafasi hii ya kuwa sehemu ya udhamini wa miongoni mwa klabu kubwa Afrika na tunahidi kwenda kutengeneza bidhaa bora kama ilivyokuwa kwa timu tulizowahi kuzivalisha kwa muda mrefu ikiwemo AS Roma ya Italy," alisema
Akizungumza kwa niaba ya Simba Kaimu Mtendaji Mkuu Zubeda Sakuru amesema ushirikiano huo unadhihirisha malengo ya Simba kuwa klabu kubwa barani Afrika
"Ushirikiano huu kati ya Simba, Jayrutty na Diadora unaonyesha ni kiasi gani klabu ya Simba inatamani kufikia malengo yake ya kuwa timu bora barani Afrika," alisema
Nae Mwenyekiti wa Simba Murtaza Mangungu amesema Simba ina malengo ya kukuwa Kimataifa na ndio maana inafanya kazi na brand kubwa duniani
"Diadora ni brand kubwa duniani na jezi zake zimewahi kuvaliwa na klabu kubwa duniani kama AS Roma na Simba inaendelea kukua ndio maana tumeamua kuvaa brand kubwa kama hii. Tutawapa ushirikiano wa kutosha na tunamuomba Mungu kuendelea kushirikiana nao kwenye maslahi ya pande zote mbili," alisema Mangungu



