Simba kuisaka fainali CAF CC leo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 27th April 2025


Simba kuisaka fainali CAF CC leo

Leo hii katika uwanja wa Moses Mabhida mjini Durban, mechi ya kukata na shoka itapigwa wakati Stellenbosch FC wakimenyana na Simba SC katika mchezo wa marudiano wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF.

Simba wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa na faida ya ushindi wa bao 1-0 walioupata katika mchezo wa kwanza uliofanyika wiki iliyopita kwenye Uwanja wa New Amaan huko Zanzibar.

Kwa ushindi au sare yoyote, Simba watafuzu kwa mara ya pili katika historia yao kucheza fainali ya michuano ya CAF.

Katika mkutano na waandishi wa habari kabla ya mechi, Kocha Mkuu wa Simba, Fadlu Davids, alisema kuwa ana imani kubwa na timu yake na ana uhakika wa kupata matokeo mazuri katika mchezo wa leo

Davids alisisitiza kuwa ni muhimu kwa Simba kufunga bao la ugenini mapema ili kuimaliza mechi hiyo na kupunguza presha.

Kwa upande wa Stellenbosch, huu ni mchezo wa kihistoria kwao, na watahitaji kucheza kwa bidii mbele ya mashabiki wao kujaribu kugeuza matokeo

Hata hivyo, haitakuwa rahisi kwao kwani imeonekana katika mechi zilizopita Simba imeimarika sana katika mechi za ugenini viungo washambuliaji Elie Mpanzu na Kibu Denis wakiwa silaha muhimu kwa Simba katika mechi hizo

Ni wazi leo Stellenbosch watalazimika kushambulia kutafuta mabao, kufunguka kwao kutatoa mwanya kwa Simba kupitia kina Mpanzu, Kibu, Ahoua na wengine kuwaadhibu

Simba inatarajiwa kupata sapoti kubwa ya mashabiki pengine kuliko wenyeji wao kwani mji wa Durban kuna Watanzania wengi ambao wamehamashika kwenda kuishangilia Simba katika mchezo huo

Stellenbosch wanatokea mji wa Cape Town hivyo nao ni kama wageni tu hapo Durban na zaidi sio timu maarufu Afrika Kusini hivyo hawana mashabiki wengi

Ni saa 9 Alasiri (saa 10 Tanzania) ndio muda ambao mtanange huo utapigwa


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.