Mtibwa Sugar imehitaji msimu mmoja tu kurejea katika ligi kuu ya NBC baada ya juzi kupata sare ya bao 1-1 dhidi ya Bigman FC kwenye Uwanja wa Ilulu Lindi
Wakata miwa hao kutoka mkoani Morogoro wamekuwa timu ya kwanza kukata tiketi hiyo huku ikisaliwa na michezo miwili mkononi kuhitimisha msimu wa 2024-2025.
Mtibwa iliyoshuka daraja msimu uliopita sambamba na Geita Gold, imepanda kufuatia Stand United kulazimishwa suluhu ugenini na Cosmopolitan.
Mtibwa Sugar imefikisha pointi 67 baada ya kucheza michezo 28, hivyo timu pekee inayoweza kuzifikia ni Mbeya City iliyoichapa Geita Gold mabao 3-2, ambapo ikishinda mechi zake zote mbili zilizobakia itafikisha pointi 68.
Kwa maana hiyo, suluhu ya Stand United inaiweka nafasi ya tatu na pointi 59 ambapo hata ikishinda michezo yake miwili iliyobakia itaishia na 65, hivyo itakuwa na kinyang'anyiro cha kuwania michezo ya 'Play-Off' kusaka tiketi ya kupanda tu
Wakati Mtibwa Sugar ikijihakikishia kurejea ligi kuu, KenGold iliyopanda daraja msimu uliopita nayo tayari imejihakikishia tiketi ya kucheza Championship msimu ujao
Β