Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Msukuma ameishauri Serikali kuifanya Bodi ya ligi ijitegemee badala ya kuwachini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Mbali na ushauri huo, Msukuma pia amemtaka Waziri wa Michezo Profesa Paramagamba Kabudi kueleza alichokutana nacho ndani kwenye kikao cha maridhiano ya Simba na Yanga ambacho kilimfikisha saa nne za usiku
Mbunge huyo ametoa kauli hiyo leo Jumatano Mei 7,2025 wakati akichangia kwenye Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka 2025/26 ambapo Wizara imeomba Sh519.66 bilioni
Msukuma amewataka viongozi wa TFF kuiga mfano wa rais mstaa wa TFF Leodgar Tenga ambaye anasema alifanya kazi nzuri inayopaswa kuigwa hata kumfanya aendelee kuheshimika kwenye tasnia ya michezo nchini
'Alifanya kazi vizuri na ni mfano wa kuigwa, muige mfano jinsi alivyoongoza anaheshimika vinginevyo mtamaliza vipindi vyenu halafu mtakuwa mahohehahe hamjulikana mlichofanya,"amesema Msukuma
Amemtaka Waziri wa Michezo Profesa Kabudi kueleza kinagaubaga nini alichokutana nacho ndani ya kikao kilichowakutanisha viongozi wa Simba na Yanga ambacho kilimuweka hadi saa nne za usiku kwani imekuwa ni fumbo wakati watu wanataka kujua
"Ulichokisikia tueleza nasi tusikie ili tukawajulishe wananchi wetu, mpira wa Simba na Yanga ndiyo furaha, lakini kunapokuwa na migogoro halafu mnakuwa kimya na sijaona mahali popote ulipotaja migogoro hiyo hata mahali pamoja wakati Mheshimiwa Rais anajua mambo ya michezo na ametoa ndege kuwapeleka Simba Morocco," amesema.



