Abuya, Mkenya aliyebadili upepo Jangwani

Joel JJ By Joel JJ β€’ 10th May 2025


Abuya, Mkenya aliyebadili upepo Jangwani

Tangu ajiunge na Yanga katika dirisha la usajili mwaka 2024, mchezaji wa kimataifa wa Kenya, Duke Abuya, amekuwa tegemeo kubwa katika safu ya kiungo ya mabingwa wa kihistoria wa Tanzania

Uchezaji wake wa kiwango cha juu na kuzoea mazingira haraka kumeimarisha nafasi yake katika kikosi cha kocha Miloud Hamdi, na kumpatia upendo kutoka kwa mashabiki na wachezaji wenzake

Abuya awali alisajiliwa na Yanga kama kiungo mshambuliaji lakini alipotua kocha Sead Ramovic alimbadilishia majukumu ya kumtumia kama kiungo mkabaji (box 2 box) na ameimarika zaidi katika eneo hilo ambalo hata Hamdi ameendelea kumtumia

Katika mechi ambazo Mganda Khalid Aucho amekosekana, Abuya na Mudathir Yahya wametumika pamoja katika eneo la kiungo huku Abuya akitumika zaidi katika kuchezesha timu akitokea kiungo cha chini

Abuya alijiunga na Yanga akitokea Singida Black Stars, akiwa tayari na jina kubwa kutokana na uwezo wake wa kudhibiti kiungo na kusaidia mashambulizi. Akiwa amechezea vilabu kama Mathare United, Kariobangi Sharks, Nkana FC, na Kenya Police FC, alikuja Yanga akiwa na tajriba na ubunifu mkubwa uwanjani

Uongozi wa Yanga pamoja na benchi la ufundi lilikuwa na imani kubwa kwamba Abuya atakuwa msaada mkubwa kwenye kampeni za ndani na kimataifa.

Abuya alicheza mechi yake ya kwanza kwa Yanga dhidi ya FC Augsburg ya Ujerumani katika mchezo wa kirafiki uliochezwa Afrika Kusini. Licha ya kipigo cha 2-1, kiwango chake kilionyesha kuwa alikuwa tayari kutoa mchango mkubwa kwa timu.

Katika fainali ya Kombe la Toyota 2024, Abuya aliibuka kuwa mmoja wa wachezaji bora kwa kusaidia Yanga kuichapa Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwa mabao 4-0. Pasi yake ya bao kwa Stephane Aziz Ki kabla ya mapumziko ilikuwa ya kuvutia na ilithibitisha ubunifu wake mkubwa.

Abuya hakuonyesha makali yake katika mechi za ndani pekee. Katika Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF), alitoa mchango mkubwa, ikiwemo kufunga bao katika ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Commercial Bank of Ethiopia (CBE), ushindi uliowasaidia Yanga kufuzu hatua ya makundi.

Katika ligi kuu ya NBC msimu huu, Abuya amepachika mabao mawili lakini pia akitoa pasi mbili za mabao

Nje ya Uwanja: Kukuza Vipaji

Mbali na soka, Abuya pia ni miongoni mwa wachezaji wanaojali maendeleo ya vijana. Alianzisha Duke Abuya Sports Academy huko Eldoret, Kenya, kwa lengo la kukuza vipaji vya soka miongoni mwa vijana. Chuo hicho kinatoa mafunzo na elimu kwa wachezaji chipukizi, na kuonyesha dhamira ya Abuya ya kuendeleza soka nchini Kenya.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.