Ikiwa zimesalia siku chache kabla ya mchezo wa mkondo wa pili wa fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAF CC) dhidi ya RS Berkane ya Morocco, hali ya sintofahamu bado imetanda juu ya wapi mechi hiyo muhimu itapigwa.
Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) limepanga mchezo huo kufanyika katika Uwanja wa New Amaan Complex, Visiwani Zanzibar, Jumapili, Mei 25, 2025 saa 12 jioni. Hata hivyo, Simba SC bado haijatoa tamko rasmi kukubali au kupinga uamuzi huo.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa klabu hiyo, Ahmed Ali, ametoa ujumbe wa kutuliza mashabiki na wanachama wa klabu, akisisitiza kuwa juhudi kubwa zinaendelea kufanyika nyuma ya pazia ili kuhakikisha Simba inapata haki na mazingira bora ya kucheza mechi hiyo ya kihistoria katika uwanja wa Benjamin Mkapa
"Habari za Jumatatu Wana Simba wenzangu. Nafahamu wengi wetu tupo kwenye sintofahamu ya uwanja wa mechi yetu ya marudiano," aliandika Ahmed.
"Taarifa tuliyotoa awali ni kuwa klabu itatoa taarifa rasmi baada ya mchezo wetu wa kwanza kule Morocco. Viongozi wetu wa mamlaka zote wanapambana kuhakikisha jema kwa Simba linapatikana"
Ahmed alisisitiza kuwa uongozi wa klabu hauwezi kupokea tu maamuzi makubwa kama haya bila kufanya juhudi za kina kutafuta suluhu stahiki.
"Mabadiliko yenye athari kubwa kama haya huwezi kuyapokea tu bila kufanya juhudi. Hivyo basi niwaombe Wana Simba tuendelee kuwa watulivu. Ndani ya kipindi kifupi kijacho tutafahamu mustakabali wetu"
Pamoja na hali hiyo ya kutokuwepo kwa uhakika juu ya uwanja wa mchezo, Ahmed amewataka mashabiki waendelee kuipa nguvu timu yao kwa maandalizi ya kuwakabili Berkane kuendelea kama kawaida.
"Hata hivyo maandalizi ya kumtapisha Berkane yaendelee kama kawaida. Tunabebaaaaaaa β iwe chini ya bahari, iwe porini, iwe juu ya mlima β popote tunabebaaaaa," alimaliza Ahmed
Kwa sasa, macho na masikio ya mashabiki wa Simba SC na wapenda soka Tanzania yako kwa uongozi wa klabu hiyo ili kutoa tamko rasmi kuhusu uwanja utakaotumika, huku matumaini yakiwa kwamba watafanikiwa kurudisha mchezo huo uwanja wa Benjamin Mkapa



