Yanga yamkomalia Sowah

Joel JJ By Joel JJ β€’ 21st May 2025


Yanga yamkomalia Sowah

Klabu ya Yanga SC inaonekana kutopoteza muda katika maandalizi ya msimu ujao wa 2025/2026, baada ya kumuuza kiungo wao nyota Stephane Aziz KI, aliyejiunga na Wydad Casablanca ya Morocco, mabingwa hao wa Tanzania Bara wamepiga hatua kubwa kwa kuhakikisha wanaboresha safu ya ushambuliaji β€” na jina la Jonathan Sowah limewekwa kwenye mstari wa mbele.

Kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, tayari mazungumzo ya siri baina ya viongozi wa Yanga na mshambuliaji huyo kutoka Ghana yamefanyika na kufikia makubaliano ya awali. Uwezekano ni mkubwa Sowah atakuwa sehemu ya kikosi cha Yanga msimu ujao, akiandaliwa mkataba wa miaka miwili

Sowah, ambaye kwa sasa anachezea Singida Black Stars, amekuwa moto wa kuotea mbali tangu alipojiunga na timu hiyo kupitia dirisha dogo la usajili mwezi Januari. Amecheza mechi 11 na kufunga mabao 11 β€” takwimu zinazothibitisha uwezo wake mkubwa wa kufumania nyavu.

Yanga, ambao wanaelekea kumuuza mshambuliaji chipukizi Clement Mzize kufuatia mvuto wake kwa vilabu vya Afrika na Ulaya, pia wanatarajia kuachana na Kennedy Musonda ambaye mkataba wake unatarajiwa kuisha mwishoni mwa msimu huu. Hii itatoa nafasi ya usajili wa mchezaji wa kigeni kwa ajili ya kumpokea rasmi Sowah.

Inadaiwa kuwa, licha ya Sowah kuwa bado na mkataba na Singida Black Stars, mshambuliaji huyo mwenyewe kipaumbele chake ni kujiunga na Yanga kwani aliwahi kusema kwamba klabu ya Yanga ni 'nyumbani kwake'

Yanga inalenga kuunda safu ya mashambulizi itakayokuwa chini ya Jonathan Sowah na Prince Dube, wakitegemewa kuibeba timu hiyo katika harakati zake za kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.