Klabu ya Singida BS imetishia haitacheza mechi ya nusu fainali ya kombe la CRDB dhidi y Simba iliyopangwa kupigwa Jumamosi May 31 endapo mchezo huo utachezeshwa na waamuzi wenye mashaka nao
Aidha klabu hiyo imeitaka Bodi ya Ligi/TFF kumchukulia hatua mwamuzi Elly Sasie kufuatia matukio ya kutoitendea haki timu hiyo katika mchezo wa ligi kuu uliopigwa juzi Jumatano katika uwanja wa KMC Complex
Akizungumza na chombo kimoja cha habari jana, msemaji wa Singida Black Stars, Hussein Massanza alisema wameiandikia barua Bodi ya ligi na wanataka kujibiwa kinyume na hivyo watajitoa kushiriki ligi kuu na michuano ya kombe la CRDB
"Baada ya kujiridhisha kuna matukio hayakuamuliwa kwa haki kwenye mchezo wetu dhidi ya Simba Sc jana,tumewasilisha barua ya malalamiko kwa mamlaka husika kwa mujibu wa kanuni na kueleza msimamo wetu kama klabu"
"Tunataka mamlaka zimchukulie hatua mwamuzi Elly Sasie kwa kile alichotufanyia katika mchezo huo. Lakini pia tumeitaka mamlaka isitupangie waamuzi ambao tuna mashaka nao kwenye mchezo wa nusu fainali kombe la CRDB dhidi ya Simba"
"Kama mamlaka hazitafanyia kazi malalamiko yetu basi tutajiondoa kushiriki ligi kuu ya NBC pamoja na kombe la CRDB. Tutatafuta kwingine ambako tutashiriki ligi inayoendeshwa kwa haki hata kama ni Zanzibar," alisema Massanza
Malalamiko hayo ya Singida BS yanajitokeza huku kukiwa na taarifa baadhi ya timu zimetishia kutocheza mechi mbili zilizosalia kuhitimisha msimu huu baada ya kutoridhishwa na mwenendo mzima wa uendeshaji wa ligi
Mpaka sasa timu zilizofikia uamuzi huo wa kususia ligi zimefika 6



