Serikali yaiachia TFF kumaliza sakata la dabi

Joel JJ By Joel JJ • 11th June 2025


Serikali yaiachia TFF kumaliza sakata la dabi

Sakata la mchezo wa Dabi ya Kariakoo unaozikutanisha Yanga dhidi ya Simba, limeingia bungeni ambapo Serikali imesema haiwezi kuingilia kwa kuwa mchezo wa mpira wa miguu una kanuni zake kitaifa na kimataifa.

Kauli hiyo imekuja baada ya swali la nyongeza liloulizwa na Mbunge wa Makete (CCM), Festo Sanga aliloliuliza leo Juni 11,2025 wakati wa kipindi cha maswali na majibu bungeni. Sanga amesema kuimarisha timu ya Taifa ni pamoja na kuhakikisha sheria na taratibu za michezo zinafuatwa.

“Ligi yetu inaelekea mwisho lakini kumekuwa na mvutano wa hizi timu mbili (Yanga na Simba) na viongozi wa TFF (Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania), ipi kauli ya serikali?” Ameuliza Sanga.

Mh Mwinjuma alisema kama ambavyo wabunge wanafahamu shughuli za mchezo wa mpira wa miguu zina mamlaka zake za kitaifa na kimataifa.

“Na tumekuwa tukisisitiza mara kwa mara Serikali kutoingilia moja kwa moja uendeshaji wa shughuli hizo ili kuepuka kuja pengine hata kufungiwa na FIFA (Shirikisho la Mpira wa Miguu la Kimataifa) katika nyakati hizi ambapo kitakwimu nchi yetu inafanya vizuri sana katika uendeshaji wa shughuli za mpira wa miguu,” amesema.

Amesema mamlaka za uendeshaji na usimamizi wa shughuli za mpira wa miguu nchini ziko chini ya TFF sambamba na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TLPB).

Amesema Serikali hata taarifa ambazo wanazitoa bungeni huwa wanapata taarifa kutoka katika mamlaka hizo kuhusu mchezo huo.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.