Afisa Habari KenGold anusurika kwenda jela

Joel JJ By Joel JJ • 12th June 2025


Afisa Habari KenGold anusurika kwenda jela

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imemhukumu, Ofisa Habari na Mawasiliano wa Klabu ya KenGold, Joseph Mkoko(34), kulipa faini ya Sh1 milioni au kwenda jela miaka miwili baada ya kupatikana na hatia ya kuomba na kupokea rushwa.

Mkoko anadaiwa kuomba rushwa ya Sh1.5 milioni kutoka kwa mchezaji wa zamani wa timu ya mpira wa miguu ya Vital’O ya Burundi, ili amsaidie kusajiliwa na timu yake ya KenGold na kupata upendeleo wa kupangwa kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo.

Hata hivyo, mshtakiwa huyo amefanikiwa kulipa faini hiyo na hivyo kukwepa kifungo cha miaka miwili jela Hukumu hiyo imetolewa leo, Jumatano Juni 11, 2025 na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Beda Nyaki, baada ya mshtakiwa huyo kukiri mashtaka yake.

Mshtakiwa huyo amekiri mashtaka yake wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili kusomewa hoja za awali, ambapo kabla ya kusomewa hoja za awali, alikumbushwa mashtaka yake kwa kusomewa upya na ndipo alipokiri mashtaka yake na mahakama hiyo kumtia hatiani.

Baada ya kutiwa hatiani, hakimu Nyaki alimhukumu. Katika kesi ya msingi, mshtakiwa anakabiliwa na kesi ya jinai namba 13138 ya mwaka 2025 yenye mashtaka mawili ya kuomba na kupokea rushwa.

Ofisa habari huyo anadaiwa kutenda makosa yake kati ya Disemba Mosi, 2024 hadi Disemba 31, 2024 eneo la Kibaha, mkoani Pwani.

Mwanaspoti


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.