Bodi ya ligi kwa kushirikiana na klabu ya Yanga na N-Card, wametangaza utaratibu wa mashabiki kuingia uwanjani katika mchezo wa ligi kuu kati ya Yanga dhidi ya Simba utakaopigwa Jumatano, Juni 25 katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Afisa Habari wa Bodi ya Ligi Karim Boimanda amesema umeandaliwa utaratibu mzuri kuhakikisha wale waliokata tiketi kwa ajili ya mechi ya mwanzo iliyopaswa kupigwa March 08 wanaingia uwanjani
"Waliokata tiketi March 08 na tiketi hizo wanazo, wao watazitumia kuingia uwanjani siku ya Jumatano, Juni 25. Kwa wale ambao walikata tiketi lakini wamepoteza kadi, kuna utaratibu maalum umeandaliwa (swap) watapatiwa msaada geti A na geti B," alisema
Nae Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Yanga Ali Kamwe amesema wanatambua umuhimu na ugumu wa mchezo dhidi ya Simba hivyo wanafanya maandalizi kikamilifu
"Yanga inafahamu ukubwa, ugumu na umuhimu wa mchezo dhidi ya Simba siku ya Jumatano. Hii ni kama zawadi kwa mashabiki kupata Kariakoo Derby yenye msisimko wa fainali"
"Sisi Yanga tuna faida mbili yaani tunahitaji ushindi au hata matokeo ya sare, huku wenzetu wakihitaji ushindi. Kwa wanachama na mashabiki wa Yanga hii ni mechi yetu kwa kuwa inakwenda kuamua hatma yetu msimu huu. Tunawakaribisha wanayanga waje kwa wingi"
"Tukiweza kuja kwa wingi tukaujaza uwanja wa Benjamin Mkapa ni jambo kubwa zaidi. Tumefanya jitihada kubwa msimu huu kuisapoti timu yetu tangu mchezo wa kwanza. Na sasa wachezaji wetu wanatuhitaji tena katika mchezo muhimu ambao tunahitaji kupata matokeo mazuri ili tuweze kutwaa ubingwa," alisema Kamwe
Hata hivyo Kamwe hakuwa tayari kuweka wazi Yanga itarudi lini Dar es salaam huku akibainisha hata taarifa za kikosi hakupewa na viongozi lakini amewahakikishia Wanachama na mashabiki kuwa siku ya Jumatano Yanga itakuwa uwanjani kucheza dhidi ya Simba



