Unaweza kusema kazi nzuri iliyofanywa na Kocha Miloud Hamdi imewapa sababu viongozi wa Yanga kumpa mkataba wa muda mrefu
Wakati Hamdi anatua Yanga kuchukua mikoba iliyoachwa na Sead Ramovic aliyetimkia CR Belouizdad, alisaini mkataba mfupi ambao umefikia tamati jana, Juni 30
Hata hivyo baada ya kuiongoza Yanga kutwaa kombe la CRDB juzi, Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alimuhakikishia ameandaliwa mkataba mpya wa muda mrefu
Akizungumza jana Jangwani jijini Dar es salaam baada ya gwaride la ubingwa, Hamdi aliwashukuru mashabiki wa Yanga akikiri upendo wao kwa timu ni wa kipekee
"Nawashukuru sana mashabiki wa Yanga, mna upendo wa kweli kwa timu yenu, mnatuunga mkono kila hatua na kila sehemu tunayokwenda"
"Nimefanya kazi katika timu nyingi kubwa lakini niwaambie nyie ni watu wa kipekee. Leo tumekutana hapa kushangilia mafanikio yetu ya msimu huu"
"Lakini niwaambie kwa aina hii ya upendo mnaotuonyesha, tutapambana ili tukutane hapa kushangilia pamoja kila msimu," alisema Hamdi
Katika mechi 21 za mashindano ambazo Hamdi ameiongoza Yanga, ameshinda mechi 20 na kutoka sare mechi 1
Ameingoza Yanga kushinda mataji matatu yaani kombe la Muungano, Ligi Kuu na kombe la CRDB



