Katika hali ya sintofahamu juu ya mustakabali wa kiungo nyota wa Yanga SC, Stephane Aziz Ki, klabu ya Al Ahly Tripoli kutoka Libya imeendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya dili hilo huku ikisubiri nafasi ya kuingia tena mezani iwapo Wydad Athletic ya Morocco itashindwa kufanikisha usajili wake, imefahamika.
Kwa mujibu wa makubaliano yaliyowekwa kati ya Yanga SC na Wydad, tarehe ya mwisho kwa klabu hiyo ya Morocco kumaliza dili la Aziz Ki ni Julai 10. Endapo hawatakamilisha makubaliano hayo ndani ya muda huo, Yanga itakuwa na uhuru wa kufanya maamuzi mengine kuhusu kiungo huyo wa kimataifa kutoka Burkina Faso, ama kumrudisha kikosini au kupokea ofa kutoka kwa vilabu vingine.
Al Ahly Tripoli bado wapo mezani
Ingawa awali walituma ofa ambayo haikufikia kiwango kilichowekwa na Yanga, Al Ahly Tripoli bado hawajakata tamaa. Vyanzo kutoka ndani ya uongozi wa Yanga vinaeleza kuwa klabu hiyo ya Libya imedokeza kuwa iko tayari kurejea na ofa mpya ya juu zaidi iwapo Wydad watashindwa kukamilisha usajili wake ndani ya muda uliopangwa.
Kwa sasa, Aziz Ki yuko mapumzikoni nchini kwao, Ivory Coast, akisubiri hatma ya mustakabali wake wa soka msimu ujao.
Yanga wapo tayari kusubiri
Wakati mashabiki wa Yanga wakifuatilia kwa karibu kinachoendelea, uongozi wa klabu hiyo unaonekana kuwa na subira huku wakipanga mikakati mbadala kuhakikisha maslahi ya klabu yanalindwa ipasavyo iwe ni kwa kurejesha huduma za Kiunga huyo mahiri au kuangalia namna ya kunufaika zaidi kifedha endapo atauzwa.
Aziz Ki ameendelea kuwa mmoja wa wachezaji wanaovutia macho mengi Afrika, kutokana na uwezo wake mkubwa alioonyesha na mchango mkubwa kwa mafanikio ya Yanga katika miaka mitatu aliyowatumikia Wananchi.Β