Saga ya usajili wa kiungo mahiri Feisal Salum ‘Fei Toto’ inaendelea kuchukua sura mpya, baada ya Klabu ya Azam Fc kuweka ngumu juu ya kumwachia nyota wao huyo. Huku Simba ikiendelea kumuwinda, Azam Fc imeweka dau kubwa, likionekana kuziba njia kwa timu zinazotamani huduma ya kiungo huyo fundi.
Kwa mujibu wa taarifa, Fei Toto tayari amefikia makubaliano binafsi na Simba, ambapo Wekundu wa Msimbazi wanamtaka kama chaguo lao la kwanza katika eneo la kiungo cha ushambuliaji, wakitaka kuimarisha safu hiyo kuelekea msimu mpya wa mashindano.
Hata hivyo, Azam Fc haionekani kutaka kumuachia kirahisi hasa baada ya ujio wa kocha mpya Frolent Ibenge. Mkuu wa Idara ya Mawasiliano wa klabu hiyo, Thabit Zakaria ‘Zakazakazi’, amesisitiza kuwa Fei Toto bado ni mali halali ya Azam, akibainisha kuwa nyota huyo ana mkataba unaoendelea kwa mwaka mmoja zaidi.
“Fei ni mchezaji wetu na bado ana mkataba. Hatuna mpango wa kumuuza. Hata hao wanaomtaka wanajua wazi hali hiyo, ndio maana hawajafanya mazungumzo yoyote rasmi nasi,” alisema Zakazakazi, akipuuzilia mbali tetesi zinazosambaa mitandaoni.
Zakazakazi ameongeza kuwa thamani ya Fei Toto imeongezeka baada ya kujiunga Azam, akisema:
“Thamani anayopata sasa ni matokeo ya muda wake Azam. Timu nyingine walikuwa hawamuoni. Azam tumemjenga kiufundi, tumempa nafasi na sasa ameweza kuonyesha uwezo wake wa kuwaongoza wenzake na kutengeneza ushindi.”
Kwa upande mwingine, taarifa kutoka ndani ya Simba zinaeleza kuwa juhudi za kuinasa saini ya kiungo huyo bado zinaendelea kwa siri kubwa. Majadiliano baina ya viongozi wa juu wa klabu hizo mbili yanadaiwa kuwa bado hai, huku Simba ikihaha kuhakikisha inampata Fei Toto kabla ya dirisha la usajili kufungwa.



