Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Yanga Ali Kamwe amesema klabu hiyo haina sababu ya kumzuia mchezaji pale anapopata ofa nzuri ya kujiunga na klabu nyingine
Kamwe ametoa kauli hiyo baada ya kile kinachojadiliwa kuhusiana na sakata la mshambuliaji Clement Mzize ambaye Yanga imepokea ofa kutoka klabu mbalimbali kwa ajili ya kumsajili
Kamwe amekanusha taarifa zinazoenezwa kuwa inambania mchezaji wao huyo asiende kucheza soka la kulipwa nje ya nchi, akibainisha kuwa klabu inaangalia zaidi maslahi ya pande zote tatu, ndipo ikubali
"Hatubanii wachezaji, hatujawahi kufanya hivyo na hatutofanya hivyo, tumeshawahi kumuuza Fiston Mayele, ambaye alikuwa mfungaji wetu bora, alikuwa mfungaji bora wa Kombe la Shirikisho, tumemuuza Stephane Aziz Ki, wote hao wakiwa kwenye ubora wao"
"Sisi kama taasisi tumepokea ofa na tumemshirikisha mchezaji, kuna ofa ambazo sisi tunakubali kabisa, lakini unakuta upande wa mchezaji unakataa unasema si ofa rafiki kwao, au mchezaji hataki kwenda kwenye nchi husika"
"Kwa hiyo si 'inshu' ya pesa peke yake, bali kuna 'inshu' ya timu, mazingira na maslahi na mara zote klabu imekuwa karibu na mchezaji kujadiliana naye vitu vyote hivyo wala si klabu ikipata pesa zake tu iwe haina inachofutilia tena kwa mchezaji, hapana, kwa mfano pia kuna dili ambazo klabu iliona hazina maslahi mazuri kwa mchezaji tukataa," alisema Kamwe.
Kamwe amefichua kuna timu moja ya Libya, ilileta pesa nyingi upande wa klabu na mchezaji pia, lakini wakaangalia historia na rekodi ya klabu, pande zote mbili zikakataa"
"Tunataka tumuuze mchezaji wetu akiwa huru, na kila upande uridhike, naamini kama mambo yatakwenda vizuri Klabu ya Yanga itatangaza kumuuza Mzize," alisema Kamwe.
Klabu ya Esperance ya Tunisia inatajwa kutuma ofa nono zaidi inayokadiriwa kufikia Tsh Bilioni 2.6, ambayo imefikia mahitaji yaliyowekwa na Yanga
Inaelezwa tayari makubaliano baina ya klabu na klabu yamefikiwa huku mchezaji nae akiridhia upande wa maslahi yake binafsi hivyo huenda Mzize akajiunga na Esperance baada ya kumalizika kwa michuano ya CHAN



