Stars kazi ni moja dhidi ya Morocco Ijumaa

Joel JJ By Joel JJ • 21st August 2025


Stars kazi ni moja dhidi ya Morocco Ijumaa

Kesho Ijumaa, Agosti 22, macho na masikio ya Watanzania yatakuwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, ambapo Taifa Stars watakabiliana na Morocco katika robo fainali ya CHAN 2024. Ni zaidi ya mechi ya mpira, ni kipimo cha hadhi ya soka la Tanzania barani Afrika.

Taifa Stars waliweka msingi mzuri hatua ya makundi. Walikusanya pointi 10, wakifunga mabao matano na kuruhusu moja pekee. Safu ya ulinzi imeonekana imara, huku nidhamu ikiwatambulisha kama moja ya timu zilizosalia safi, hakuna kadi nyekundu.

Hii ni sura ya timu inayocheza kwa mpangilio, inalinda matokeo na kuamua pale inapopata nafasi. Ni sababu ya mashabiki wengi kuamini kwamba kesho Stars wana kila kitu cha kusimama imara mbele ya mabingwa wa zamani.

Morocco si wageni kwenye hatua hizi. Wamewahi kutwaa CHAN mara mbili na safari yao mwaka huu imethibitisha ubora wao wa kushambulia. Waliibuka washindi dhidi ya Angola (2-0), Zambia (3-1), na DR Congo (3-1), wakafunga jumla ya mabao manane.

Hata hivyo, walipoteza mchezo muhimu dhidi ya Kenya (1-0), jambo linaloonyesha kuwa wanaweza kushindwa wanapobanwa.
Safu yao ya mbele ni hatari, lakini ukuta wao bado una mashimo, jambo linalowapa Stars tumaini la kupata nafasi 

Unaweza kusema ni mpambano wa falsafa mbili: Stars wakitegemea uimara wa ulinzi na nidhamu, Morocco wakiwa na silaha ya mashambulizi makali.

Faida kwa Tanzania ni kucheza mechi hiyo dimba la Benjamin Mkapa. Mpaka sasa zaidi ya mashabiki 40,000 wana uhakika wa kushuhudia mchezo huo baada ya wadau mbalimbali kununua tiketi. Wanasema shabiki ni mchezaji wa 12 uwanjani, Stars inawahitaji Watanzania kujaza dimba la Mkapa

Kwa Taifa Stars, huu ni wakati wa kuonyesha dunia kuwa Tanzania si mgeni tena kwenye jukwaa kubwa. Morocco wanakuja na historia ya ubabe, lakini Stars wanaingia na kitu ambacho si rahisi kupewa, imani ya taifa lote.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.