Fadlu kujiuliza kwa Gaborone United

Joel JJ By Joel JJ β€’ 17th September 2025


Fadlu kujiuliza kwa Gaborone United

Kikosi cha Simba kimeondoka jijini Dar es salaam mapema leo kuelekea Botswana ambako wanakabiliwa na mchezo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Gaborone United

Mchezo huo unatarajiwa kupigwa siku ya Jumamosi, Septemba 20 huko Botswana majira ya saa 2 usiku

Baada ya kupoteza mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga jana, ni wazi Kocha Fadlu Davids na benchi lake la ufundi hawahitaji kupoteza mchezo huo ugenini kwani matokeo hayo yanaweza kuongeza presha juu ya hatma yake

Mabosi wa Simba hawakufurahishwa na matokeo ya mchezo dhidi ya Yanga hivyo ni kama wamempa mtihani Fadlu ahakikishe anaipeleka Simba hatua ya makundi ya michuano ya ligi ya mabingwa

Akizungumza muda mfupi kabla ya kikosi kuondoka nchini mapema leo, Fadlu alisema wanakwenda Botswana kupambana, lengo ni kupata matokeo mazuri ambayo yatawaweka katika nafasi nzuri ya kutinga raundi ya kwanza katika mchezo wa marudiano ambayo utapigwa Septemba 27 uwanja wa Benjamin Mkapa

"Hii ni ligi ya mabingwa, kila timu unayoiona inashiriki michuano hii ni bora katika nchi husika. Tunajua Gaborone United watahitaji kufanya vizuri katika uwanja wao wa nyumbani, haitakuwa mechi nyepesi lakini tumeweka malengo"

"Tunahitaji kupata matokeo mazuri ambayo yatatuweka katika nafasi ya kusonga mbele kwenye mechi ya marudiano itakayochezwa wiki ijayo uwanja wa Benjamin Mkapa," alisema

Msimu huu Simba imeweka malengo makubwa katika michuano yote inayoshiriki, kushinda mataji ya ndani na kufanya vyema zaidi katika michuano ya ligi ya mabingwa baaada ya mafanikio waliyopata kwenye kombe la Shirikisho msimu uliopita kwa kucheza fainali


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.