Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola amekiri mambo yameharibika katika kikosi chake ikiwa ni siku chache tu baada ya kutabiriwa angejiuzulu nafasi yake kama kocha wa timu hiyo wiki hii.
Man City ilipoteza kwa mabao 3-1 dhidi ya timu ya Norway, Bodo/Glimt, katika Ligi ya Mabingwa Ulaya, Jumanne na kuendelea kushuka katika msimamo wa michuano hiyo.
Matokeo hayo yamesababisha vijana hao wa Guardiola kuwa katika hatari ya kushuka kutoka kwenye nafasi za kufuzu moja kwa moja na inaweza kujikuta ikicheza mechi ya mtoano ili kufuzu hatua ya 16 bora.
Kipigo hicho mbele ya Bodo, kilikuja ikiwa ni siku chache tu tangu kupoteza dabi ya Manchester dhidi ya wapinzani wao Man United kwa mabao 2-0.
Man City ambayo pia ipo katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu England, kwa sasa haijashinda mechi tano kati ya saba ilizocheza hivi karibuni katika mashindano yote.
“Leo ilikuwa fursa nzuri kwetu ya kusogea juu katika msimamo, lakini haijawa kama tulivyotarajia. Kwa sasa inaonekana kila kitu kinakwenda vibaya na kinaenda kinyume na sisi," alisema Guardiola.
“Huo ndiyo ukweli na lazima tujaribu kubadilisha hali hii. Tulijaribu kufanya tulivyoweza ingawa naamini katika mashindano haya hatujafanya zaidi. Man United walikuwa bora zaidi kuliko sisi (Jumamosi). Leo ilikuwa ni kasi ya mchezo ndio iliyotuadhibu.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, mwandishi wa habari kutoka kituo cha Bein, Richard Keys alisema siku za Guardiola zimeshamalizika na alidai angeondoka kabla ya mechi hiyo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
“Anaweza akaondoka wiki hii na atakapoondoka tu, kocha wa zamani wa Chelsea, Enzo Maresca atapewa mikoba na ataonekana rasmi Uwanjani katika mechi ya ligi wikiendi ijayo dhidi ya Wolves."
“Inawezekana Man City wenyewe wakawa hawataki kusikia taarifa hii lakini huo ndio ukweli. Hii iko kwenye akili yake na nimeambia hajabadilisha mawazo."
Guardiola anaamini moja kati ya mambo ambayo yamechangia sana timu yake kuwa katika kiwango kibovu ni tatizo la majeraha ambalo lipo katika safu yake ya ulinzi.



