Mbappe aendeleza rekodi ya mabao La Liga

Joel JJ By Joel JJ • 25th January 2026


Mbappe aendeleza rekodi ya mabao La Liga

Klabu ya Real Madrid iliendeleza mwendo wake mzuri kwenye Ligi Kuu ya Hispania (La Liga) baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Villarreal katika mchezo uliochezwa Jumamosi, Januari 24, 2026, kwenye uwanja wa Estadio de la Ceramica.

Katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa hasa kipindi cha kwanza, Real Madrid walionyesha ubora wao wa uzoefu na nidhamu ya hali ya juu, kabla ya mshambuliaji nyota Kylian Mbappe kuamua hatima ya mchezo kwa kufunga mabao yote mawili.

Baada ya dakika 45 za kwanza kumalizika bila mabao, Real Madrid walirejea kipindi cha pili wakiwa na kasi zaidi. Mbappe alifungua ukurasa wa mabao dakika ya 47 akitumia pasi ya Vinicius Júnior, akimalizia kwa shuti la uhakika lililomshinda kipa wa Villarreal.

Villarreal walijaribu kurejea mchezoni kwa kuongeza mashambulizi, lakini safu ya ulinzi ya Real Madrid iliyoongozwa kwa umakini mkubwa iliweza kudhibiti presha hiyo. Mwishoni mwa mchezo, Mbappe alihitimisha ushindi wa Los Blancos baada ya kufunga bao la pili kwa mkwaju wa penalti, kufuatia yeye mwenyewe kuchezewa vibaya ndani ya eneo la hatari.

Ushindi huo umeongeza ari na kujiamini kwa Real Madrid katika mbio za kuwania ubingwa wa La Liga, huku Mbappe akiendelea kuthibitisha thamani yake kama mmoja wa wachezaji muhimu zaidi kikosini msimu huu. Kwa upande wa Villarreal, matokeo hayo yamewaacha wakitafakari namna ya kuboresha safu yao ya ushambuliaji katika mechi zijazo.

Kwa matokeo ya Jumamosi, Real Madrid wamepanda katika nafasi kwanza kwenye msimamo wa ligi, wakionesha dhamira yao ya kutwaa taji la La Liga msimu wa 2025/26, huku Villarreal wakilazimika kurejea upya kwenye ratiba ngumu inayowakabili mbele.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.