Klabu ya Raja Casablanca ya Morocco inaripotiwa kuanza hatua za awali za kumnyemelea kiungo wa Young Africans SC (Yanga), Moussa Balla Conte, baada ya kuwasilisha ofa ya kutaka kumsajili nyota huyo raia wa Guinea.
Awali, Yanga ilikuwa na mpango wa kumtoa Conte kwa mkopo ili kumpa nafasi ya kupata muda zaidi wa kucheza, hasa baada ya mwanzo mgumu alioupata tangu ajiunge na kikosi hicho.
Hata hivyo, mpango huo unaonekana kubadilika kwa kasi baada ya mchezaji huyo kuanza kuonyesha makali yake uwanjani, hali iliyomfanya kupata imani zaidi kutoka kwa benchi la ufundi.
Pamoja na kuimarika kwake, uongozi wa Yanga sasa unakabiliwa na maamuzi magumu kuhusu hatma ya Conte, hasa ikizingatiwa kuwa mchezaji mwenyewe anaonesha nia ya kujiunga na Raja Casablanca, akitafuta mwanzo mpya baada ya changamoto alizokutana nazo mwanzoni mwa safari yake Jangwani.
Raja Casablanca kwa sasa inanolewa na Fadlu Davids, aliyekuwa kocha wa Simba SC kabla ya kuondoka mwanzoni mwa msimu huu. Uwepo wa Fadlu katika benchi la Raja unaongeza mvuto wa dili hilo, hasa ikizingatiwa kuwa kocha huyo alikuwa akimtamani Conte hata wakati alipokuwa akiinoa Simba.
Ikumbukwe kuwa wakati Yanga inamsajili Conte kutoka klabu ya CS Sfaxien ya Tunisia, kulikuwa na ushindani mkali kutoka kwa Simba, ambao nao walikuwa tayari kumsajili mchezaji huyo. Hata hivyo, Yanga iliibuka na saini yake, jambo lililochukuliwa kama ushindi mkubwa katika soko la usajili.
Kwa sasa, Yanga inadaiwa imefunga shughuli zake za usajili katika dirisha hili, hali ambayo inaweza kufanya iwe vigumu kumruhusu Conte kuondoka kwa haraka, isipokuwa kuwe na makubaliano maalum yatakayoridhisha pande zote.