Wachezaji wa timu ya taifa ya Morocco, Achraf Hakimi na Ismael Saibari, wamelazimika kufika mbele ya Kamati ya Nidhamu ya CAF kutoa maelezo na kujitetea kuhusiana na matukio yaliyojitokeza katika fainali ya AFCON 2025.
Matukio hayo yalianza baada ya wawili hao, kwa nyakati tofauti, kuonekana wakiondoa taulo la kipa wa Senegal, Edouard Mendy, upande wa goli na kulirusha pembeni ya mashabiki, jambo lililosababisha taharuki na mijadala mikali miongoni mwa mashabiki na vyombo vya habari.
Kamati ya Nidhamu ya CAF imeanza uchunguzi wa kina ili kubaini ukweli wa matukio hayo na kuamua hatua stahiki za kisheria na kiadabu. Uamuzi wa kamati hiyo unatarajiwa kutolewa ndani ya saa 48 zijazo, na unaweza kuwa na athari si tu kwa wachezaji hao, bali pia kwa viwango vya nidhamu, uwajibikaji, na mustakabali wa soka barani Afrika.
Mashabiki na wadau wa soka wanangojea kwa hamu kuona hatua itakayochukuliwa. Wengi wanataka kuhakikisha kuwa uamuzi utakuwa wa haki, ukizingatia viwango vya uwajibikaji na nidhamu katika michezo ya kimataifa.
Matokeo yake yanatarajiwa kuwa alama muhimu kwa wachezaji wote wa kimataifa kwamba hatua zisizofaa au za hila katika uwanja wa michezo hazitavumiliwa.
CAF pia inatarajiwa kuchukua hatua juu ya matukio yote yaliyogubika mchezo mzima kuanzia kitendo cha Senegal kususia mchezo baada ya Morocco kupewa mkwaju wa penat dakika za lala salama na baadae kurejea tena uwanjani kumaliza mchezo ambao walishinda kwa bao 1-0 na kutwaa taji la Afcon 2025.
Kocha mkuu wa Senegal, Pape Thiaw, pamoja na wachezaji wake Iliman Ndiaye na Ismaila Sarr, nao walifikishwa mbele ya kamati ya nidhamu ya CAF kuhusiana na matukio yaliyotokea katika mechi hiyo. Kocha huyo na wachezaji wake wanatuhumiwa kwa utovu wa nidhamu waliouonyesha wakati wa mechi hiyo, iliyopigwa Januari 18, 2026 mjini Rabat



