Bodi ya ligi yafunguka Kariakoo Dabi kupelekwa Zanzibar

Joel JJ By Joel JJ β€’ 20th February 2026


Bodi ya ligi yafunguka Kariakoo Dabi kupelekwa Zanzibar

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) imeeleza sababu za kuhamisha Dabi ya Kariakoo kati ya Yanga Sc na Simba Sc kutoka Uwanja wa Benjamin Mkapa Stadium hadi New Amaan Complex, Zanzibar

Mchezo huo namba 54 wa Ligi Kuu ya NBC unatarajiwa kuchezwa Machi 1, 2026, visiwani Zanzibar badala ya Dar es Salaam kama ilivyopangwa awali.

Akizungumza kuhusu mabadiliko hayo, Afisa Habari wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Karim Boimanda, amesema sababu kuu ya kuhamisha mchezo huo ni kutokana na Uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa na matumizi mengine siku hiyo.

Kwa mujibu wa Boimanda, Machi 1, 2026 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa kutafanyika mashindano makubwa ya Mabara yote ya Qur'an ulimwenguni, tukio litakalohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa na kimataifa. Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Hussein Mwinyi.

Kumekuwa na taarifa kuwa klabu ya Simba iliandikia barua Bodi ya Ligi kuhoji mabadiliko hayo ya uwanja, wakidai hawakupata taarifa rasmi ndani ya muda wa kikanuni kuhusu uamuzi huo.

Bodi ya Ligi imesisitiza kuwa uamuzi wa kuhamisha dabi hiyo umefanyika kwa kuzingatia ratiba na upatikanaji wa viwanja, huku ikihakikisha mchezo huo utachezwa kwa tarehe iliyopangwa lakini katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Dabi ya Kariakoo ni mechi kubwa yenye mvuto zaidi katika Ligi Kuu Tanzania Bara, na uamuzi wa kuipeleka Zanzibar unatarajiwa kuongeza hamasa kwa mashabiki wa soka visiwani humo.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.