Mosemane afungua milango Mamelodi Sundowns

Joel JJ By Joel JJ β€’ 20th February 2026


Mosemane afungua milango Mamelodi Sundowns

Kocha maarufu wa Afrika Kusini, Pitso Mosimane, ameweka wazi uwezekano wa kurejea kuinoa klabu ya Mamelodi Sundowns, kufuatia ripoti zinazoeleza kuwepo kwa mazungumzo kati yake na uongozi wa timu hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali za michezo nchini Afrika Kusini, Sundowns inadaiwa kuchunguza uwezekano wa kufanya mabadiliko ya benchi la ufundi, hali iliyochochea tetesi za kurejea kwa Mosimane, kocha aliyewahi kuipa klabu hiyo mafanikio makubwa katika historia yake.

Mosimane aliiongoza Sundowns kwa mafanikio makubwa ikiwemo kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 2016 pamoja na mataji kadhaa ya Ligi Kuu ya Afrika Kusini (PSL). Rekodi hiyo imeendelea kumfanya kuwa miongoni mwa makocha wanaoheshimika zaidi barani Afrika.

Ripoti hizo zinakuja wakati kukiwa na sintofahamu kuhusu mustakabali wa kocha wa sasa, Miguel Cardoso, ingawa klabu haijatoa tamko rasmi kuhusu mabadiliko yoyote ya kiufundi.

Hata hivyo, Mosimane mwenyewe hajathibitisha rasmi kurejea kwake, lakini katika mahojiano mbalimbali amesisitiza kuwa hana kinyongo na klabu hiyo na yuko tayari kusikiliza fursa zitakazosaidia maendeleo ya soka.

Iwapo makubaliano yatafikiwa, kurejea kwa Mosimane kutachukuliwa kama hatua kubwa kwa Sundowns, hasa katika kipindi hiki ambacho ushindani wa ndani na kimataifa unaendelea kuongezeka.

Hadi sasa, uongozi wa Mamelodi Sundowns haujatoa taarifa rasmi kuthibitisha au kukanusha mazungumzo hayo, huku mashabiki wakisubiri kwa hamu uamuzi wa mwisho.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.