Mustakabali wa kocha mkuu wa Azam FC, Florent Ibenge, umeanza kuibua mjadala mzito ndani na nje ya Tanzania baada ya taarifa kueleza kuwa anawaniwa na mataifa mawili ya Afrika kwa ajili ya kuinoa timu zao za taifa.
Kwa mujibu wa taarifa zinazoibuka kutoka Afrika Magharibi, Shirikisho la Mpira wa Miguu Burkina Faso (FBF) linamtazama Ibenge kama moja ya makocha wanaoweza kuinoa timu ya taifa ya nchi hiyo.
Kipaumbele cha kwanza kwa sasa kinatajwa kuwa ni kocha wa Ghana, James Kwesi Appiah, lakini endapo mazungumzo hayatofikia muafaka, jina la Ibenge linawekwa mezani kama chaguo la pili lenye uzito.
Ibenge anawekwa kwenye orodha ya makocha watano wanaotajwa kuweza kurithi mikoba ya Brama Traore, jambo linaloonyesha namna ambavyo thamani yake kiufundi inazidi kupaa barani Afrika.
Hii si mara ya kwanza kwa kocha huyo kuhusishwa na majukumu ya timu za taifa, hasa kutokana na uzoefu wake mkubwa na mafanikio aliyowahi kuyapata huko nyuma.
Wakati Burkina Faso wakiendelea kupima upepo, taarifa kutoka Angola nazo zimeongeza presha kwa mabosi wa Azam FC. Vyanzo mbalimbali nchini humo vinaeleza kuwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Angola (FAF) limeanza mazungumzo rasmi na Florent Ibenge kwa lengo la kumteua kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya taifa ya Angola.
Endapo mazungumzo hayo yatazaa matunda, Ibenge anatarajiwa kurithi nafasi iliyoachwa wazi na Patrice Beaumelle, ambaye aliachana na timu hiyo hivi karibuni.
Hali hii inaifanya Azam FC kujikuta katikati ya presha kubwa. Kwa wakati mmoja, kocha wao mkuu anagombaniwa na mataifa mawili yenye historia na ushindani mkubwa wa soka barani Afrika.
Hili si jambo la kubezwa, hasa ukizingatia kuwa timu za taifa mara nyingi huja na ofa zenye mvuto mkubwa, si tu kifedha bali pia hadhi na fursa ya kushiriki mashindano makubwa ya kimataifa.
Kwa mtazamo wa kiushindani, kumpoteza Ibenge katika kipindi hiki kunaweza kuwa pigo kwa Azam FC, hasa kama klabu hiyo ina malengo makubwa ya ndani na kimataifa.
Uongozi wa klabu hiyo unapaswa kutumia nguvu kubwa, kimkakati na kifedha, kuhakikisha unamlinda kocha wao dhidi ya mvuto wa benchi za timu za taifa.
Swali kubwa linalobaki ni je, Azam FC wataweza kumshawishi Ibenge kubaki Chamazi, au ndoto ya kuiongoza timu ya taifa itamvuta nje ya Tanzania?