Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker ameweka wazi mkakati wake wa kuboresha eneo la umalizia kwa kikosi chake ili kuhakikisha wanatumia vyema nafasi na kufunga mabao mengi.
Barker amesema wanahitaji kuongeza ufanisi mbele ya lango kwani wanatengeneza nafasi nyingi lakini matumizi ya nafasi hizo sio kwa kiwango kikubwa.
Kocha huyo raia wa Afrika Kusini amesema katika ligi yenye ushindani kama hii ya Tanzania Bara, wakati mwingine uwiano wa mabao unaweza kuamua bingwa.
"Nimefurahishwa na ushindi dhidi ya Prisons lakini ukweli ni kwamba tunatengeneza nafasi nyingi na hatuzitumii ipasavyo. Lazima tuwe na makali zaidi mbele ya lango, napenda kumaliza mechi mapema."
"Timu inaendelea kuimarika na ninaamini tutaendelea kufanya vizuri zaidi ya sasa, nina furaha kuona vijana wakipambana kila mmoja katika nafasi yake, akionyesha vile anaweza kuwa msaada kwa timu."
"Wakati mwingine ubingwa unaamuliwa kwa tofauti ya mabao, hivyo hatupaswi kuridhika na ushindi wa bao moja au mawili kama kunakuwa na nafasi za kufunga zaidi,β alisema Barker
Tangu achukue majukumu ya kuinoa Simba, kikosi chake kimefunga mabao matatu katika mechi moja tu ya kombe la CRDB dhidi ya Greenland huku wakicheza mechi saba mfululizo bila ya kupoteza



