CAF yaboresha kanuni sifa za makocha

Joel JJ By Joel JJ β€’ 25th February 2026


CAF yaboresha kanuni sifa za makocha

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeanzisha kanuni mpya kwa makocha wa timu zinazoshiriki mashindano yote yanayodhibitiwa na shirikisho hilo, hatua inayotarajiwa kuathiri soka la klabu na timu za taifa hapa Tanzania.

Kulingana na kanuni mpya, kocha msaidizi atakayekalia benchi katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Kombe la Shirikisho, au mashindano ya timu za taifa za wanaume lazima awe na leseni Daraja A au Pro ya CAF, au leseni ya Pro kutoka shirikisho jingine la soka la bara.

Hii inabadilisha kanuni za awali ambapo kocha msaidizi aliweza kukaa benchi akiwa na leseni ya Daraja B ya CAF au A kutoka shirikisho jingine.

Kwa mashindano ya wanawake wakubwa na mashindano ya klabu za wanawake, kocha msaidizi anaweza kuwa na leseni ya Daraja B ya CAF, isipokuwa anatoka shirikisho jingine, basi lazima awe na leseni la Pro.

Timu za vijana za wanaume zinapaswa kufundishwa na kocha mwenye leseni A ya CAF, huku msaidizi akiwa na Daraja B; kwa timu za wanawake, kocha mkuu anatakiwa kuwa na leseni B ya CAF au A kutoka shirikisho jingine, na msaidizi awe na leseni C ya CAF au A kutoka shirikisho jingine.

Aidha, timu zinazoshiriki mashindano ya wanawake za CAF lazima ziwe na angalau mmoja kati ya kocha mkuu au msaidizi kuwa mwanamke, hatua inayolenga kuendeleza usawa wa kijinsia katika soka.

Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Oscar Mirambo, amesema kwamba masharti haya yatatekelezwa kwenye kanuni za mashindano ya hapa nchini, lakini TFF italazimika kuandaa maandalizi maalum ya kiuwezeshaji kwa makocha ili kuhakikisha wanakidhi vigezo vipya.

Uamuzi huu wa CAF unalenga kuimarisha taaluma ya makocha barani Afrika na kuhakikisha timu zote zinashikiliwa na viongozi wenye sifa zinazohitajika.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.